Get Even More Visitors To Your Blog, Upgrade To A Business Listing >>

HOFU ILIYOPITILIZA HUANZIA UTOTONI, KUATHIRI UFANISI KAZINI




Mwili wa mwanadamu ni moja ya mashine kubwa na ngumu kujifunza inavyofanya kazi, wanadamu tumeumbwa Kuwa na Hofu au wasiwasi kama sehemu ya kujihami na matukio ya kila siku tunayokutana nayo.
Lakini hofu ina kiwango chake ambapo inapopitiliza inaweza kuwa ni tatizo linalohitaji matibabu na ushauri.
Wataalam wa afya ya akili wanaitambua hofu au wasiwasi uliokithiri kama Generalised Anxiety Disorder (GAD).  Tatizo hili huwakosesha ajira baadhi ya watu kutokana na kutojiamini katika usaili wa kazi au wanafunzi wanaofanya mitihani.
Hofu iliyopitiliza huambatana na wasiwasi kupita juu ya maisha ya kila siku pamoja na matukio yake bila mhusika kuwa na sababu maalum ya kuwa na hofu hiyo.
Watu wenye kuhisi hofu kubwa bila sababu yoyote ya msingi ya kuwafanya wawe hivyo.  Mara nyingi watu wenye tatizo hili huhisi janga kubwa litawatokea karibuni au maafa yatawakumba katika maisha yao na daima hawaachi kuwa na hofu juu ya familia zao, fedha, afya, ajira, masomo, au biashara zao.
Maisha yao ya kila siku huwa na mchanganyiko wa hofu, wasiwasi na huzuni, kiasi kwamba hatimaye hofu hutawala mawazo ya mhusika na kuingilia ufanisi wake kazini, kwenye masomo, shughuli za kijamii au uhusiano na mwenza wake.
Inakadiriwa watu wazima milioni nne mpaka tano nchini Marekani hukumbwa na tatizo hili kila mwaka.  Hapa nchini hakuna takwimu zinaonesha ukubwa wa tatizo hili.
Kwa kawaida, wanawake huathiriwa zaidi kuliko wanaume.  Aidha hofu iliyopitiliza mara nyingi huanza kipindi cha utoto mara nyingi kabla ya ujana ingawa inaweza kutokea ukubwani.
Dalili
Hofu isiyo na kikomo huathiri uwezo wa mtu kufikiri ingawa baadaye humletea matatizo ya kiafya.  Hali hii inaweza kuambatana na dalili mbalimbali siyo tu zinazohusu kufikiri na akili bali utendaji kazi wa mwili.
Baadhi ya dalili hizo ni kuwa na hisia ya kuwepo kwa janga, kwamba kitu kibaya kitatokea muda wowote na hatari inamnyemelea mhusika.
Hofu kuu, kujihisi kutaka kukimbia, kuondoka mbali na hatari hiyo.
Rangi ya ngozi kuwa ‘nyeupe’ kama mtu aliyeishiwa damu au kuhisi ngozi kuwaka moto na koo kubana.
Wengine huhisi kama koo limefunga au wamekabwa na kitu kooni, kuchanganyikiwa, kuhisi kutengwa na ulimwengu, kupoteza hisia, kutojitambua mwenyewe, kuhisi kizunguzungu na kichwa kuuma kuwa chepesi.
Wapo wanaopepesuka wanapotembea au kuwa mvurugo wa hisia, hofu ya kurukwa akili na kupoteza uwezo wa kujidhibiti.  Nyingine ni kuhisi kama vile kuna kitu kinachobana kichwani (kama uliyezungushiwa Kamba au rubberband), kujihisi baridi au joto kali ingawa hali ya hewa yaweza kuwa ya kawaida.
Dalili nyingine ni kushindwa kujituliza, kuhisi kitu kinakaba tumboni, kichefuchefu, ganzi au kuchomachoma sehemu Fulani za mwili na kuziba masikio na mapigo ya moyo kudunda kwa kasi.
Moyo kwenda kasi isivyo kawaida, maumivu makali kifuani, shingoni, kwenye mabega, kichwani au usoni ni dalili nyingine za kuzingatia.  Kuhisi kukosa hewa au kupumua kwa shida na kutokwa jasho.
Kubanwa kifua, kutetemeka iwe ndani kwa ndani au kunakoonekana na watu wengine, kuchafuka tumbo, kuhisi haja ndogo au kubwa mara kwa mara, kutapika, uchovu wa mara kwa mara, kupata usingizi kwa shida au kulala usingizi wa mang’amung’amu.
Sababu
Chanzo halisi cha hofu kupita kiasi hakifahamiki.  Hata hivyo kuna baadhi ya vitu ambavyo vimegundulika kuwa vinachangia kuwepo kwa tatizo hili miongoni mwa watu.
Vitu au mambo hayo ni pamoja na vinasaba au genetics.  Baadhi ya utafiti unaonesha vinasaba vina nafasi kubwa ya kumfanya mtu wa familia yenye matatizo ya kuwa na hofu iliyopitiliza naye kuwa na uwezekano mkubwa wa kuyapata.  Hii inamaanisha, hofu iliyopitiliza inaweza kurithiwa miongoni mwa wanafamilia.
Mfumo wa kemikali za ubongo ni sababu nyingine.  Kuwepo kwa hofu iliyopitiliza kumehusishwa na kuwapo kwa kiwango kisicho sahihi cha baadhi ya kemikali zinazosaidia kusafirisha taarifa katika ubongo yaani neurotransmitters.
Kazi ya kemikali hizi ni kupitisha taarifa na ujumbe kutoka Seli moja ya neva mpaka seli nyingine.  Iwapo kemikali hizi zitakuwa katika kiwango kisicho sahihi ama kupungua au kuongezeka, taarifa hazitaweza kusafirishwa kama kawaida na kutoufikia ubongo.  Hali hii inaweza kusababisha mabadiliko katika utendaji kazi wa ubongo na hatimaye mhusika kupatwa na hofu iliyopitiliza.
Mazingira.  Inaelezwa, matukio kama vile ajali, kuumia au matukio yenye msongo mkubwa kama vile kunyanyaswa kwa namna yeyote ile, kufiwa na mtu unayempenda, talaka, kufukuzwa kazi huweza kuwa chanzo cha hofu iliyopitiliza.
Wanafunzi wanaobadilisha au kufukuzwa shule wanaweza kuwa na hofu iliyopitiliza.  GAD huwa mbaya mhusika anapokuwa na msongo wa mawazo.  Aidha, matumizi ya vilevi kama vile pombe, sigara hata kahawa yanaweza kuchangia tatizo hili.
Waliowahi kuwa watumiaji wakubwa wa vitu hivyo kisha wakaacha ghafla, wapo kwenye hatari ya kukumbwa na tatizo hili pia.
Vipimo na uchunguzi
Kabla ya kumfanyia uchunguzi wa mwili mzima kufahamu kama hana tatizo jingine la mwili linaweza kumletea dalili za hofu iliyopitiliza, daktari anapaswa kufahamu historia ya mgonjwa.
Iwapo daktari atabaini mgonjwa alikuwa akisumbuliwa na dalili hizi kwa muda mwingi yaani miezi sita au Zaidi, ni Dhahiri ana GAD.  Dalili hizi ni lazima ziingilie na kuathiri maisha ya kila siku.
Pamoja na kuwa hakuna kipimo cha kuweza kugundua ugonjwa huu, daktari pia anaweza kuagiza kufanyika kwa vipimo vingine ili kuchunguza iwapo mgonjwa ana tatizo jingine lolote la kiafya.
Matibabu
Iwapo uchunguzi utaonesha mgonjwa hana tatizo jingine lolote mwilini, daktari wa masuala ya afya ya akili atatakiwa kumhudumia.  Matibabu yake kwa kawaida hujuisha dawa na tiba ya kujitambua yaani cognitive-behavioral therapy.
Hofu iliyopitiliza haina ya moja kwa moja.  Hata hivyo kuna baadhi ya mambo ambayo hutumika kupunguza makali yake.  Mambo hayo ni pamoja na kuacha au kupunguza matumizi ya baadhi ya vyakula au vinywaji kama vile kahawa, chai, cola au chokleti.
Kufanya mazoezi mep[esi ya mwili ikiwamo kutembea, kukimbia na kuogelea kila siku angalau kwa nusu saa na kutafuta ushauri nasaha pindi unapoumizwa moyo au nafsi ni mambo yanayoshauriwa.


This post first appeared on Afya Na Kiasi, please read the originial post: here

Share the post

HOFU ILIYOPITILIZA HUANZIA UTOTONI, KUATHIRI UFANISI KAZINI

×

Subscribe to Afya Na Kiasi

Get updates delivered right to your inbox!

Thank you for your subscription

×