Na Allan Vicent, Tabora
MAPISHI ya Vyakula Vya Asili yamekuwa kivutio katika maonesho ya maadhimisho ya Siku ya Lishe Duniani yanayofanyika kwenye Uwanja wa Nane Nane uliopo Ipuli, Tabora.
Maonesho hayo yamezinduliwa jana na Mkoa huo Dk. Batilda Burian, ambaye ameitaka jamii kuwa na utamaduni wa kula Vyakula Vya asili kutokana na virutubisho vyake vinavyosaidia kuimarisha afya.
Batilda amesema elimu ya lishe ni muhimu kwa kuwa itasaidia jamii kutambua umuhimu wa kula vyakula vyenye virutubisho vya kutosha na kuacha kupika chakula kwa mazoea.
Amesema lishe bora inapaswa kuwa agenda ya kudumu na kuhubiriwa katika mikutano yote inayofanyika katika halmashauri za mkoa huo ili kupunguza matatizo yatokanayo na lishe duni.
Amefafanua kuwa ulaji vyakula visivyo na lishe huchangia kwa kiasi kikubwa tatizo la udumavu kwa watoto walio na umri chini ya miaka mitano na kinamama wajawazito kujifungua watoto wasio na afya njema.
“Wakuu wa wilaya na wataalamu wa halmashauri hamasisheni jamii kutumia vyakula Vya Asili kwa kuwa vina virutubisho vya lishe bora ambavyo vitawapa afya njema na nguvu za kufanya kazi,” amesema.
Aidha amewapongeza akinamama wa mkoa huo kwa kuandaa vyakula vya asili ili kuonesha uhalisia wa vyakula vyenye virutubisho vya lishe ambavyo vimeungwa na karanga, nazi na viungo vingine.
Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Tabora Dk. Yahaya Nawanda amemhakikishia mkuu wa mkoa kuwa watatekeleza maelekezo yote aliyowapa ikiwamo kuhamasisha jamii kutumia lishe yenye virutubisho kamili.
Maadhimisho hayo yanatarajiwa kufikia tamati Oktoba 23,2021, mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dk Doroth Gwajima.
The post Mapishi vyakula vya asili ya kivutio Tabora appeared first on News Africa Now.