Get Even More Visitors To Your Blog, Upgrade To A Business Listing >>

Watoto Mkoani Iringa Wapigwa Marufuku Kutembea Saa 12 jioni na Kuendelea

Tags: alisema watoto

INNOCENT-THE BLOGGER-BOY

Serikali wilayani Iringa imetoa waraka unaozuia Watoto wenye umri wa kuanzia miaka 14 kushuka chini, kutotembea usiku kutokana na kukithiri kwa vitendo vya ulawiti na ubakaji.

Wiki moja iliyopita wananchi walimpiga hadi kumuua kijana aliyefahamika kwa jina moja la Emmanuel (25-30), baada ya kukutwa akimbaka mtoto mwenye umri wa miaka kumi, katika eneo la Mtwivila, Manispaa ya Iringa.

Pia, katika kipindi cha miezi mitatu iliyopita matukio 36 ya ubakaji yameripotiwa kutokea manispaa hiyo huku watuhumiwa 17, wakitiwa mbaroni.

Mkuu wa Wilaya ya Iringa, Richard Kasesela Alisema hali ni mbaya hivyo kila mzazi na mlezi anapaswa kumlinda mtoto wake.

Kasesela alisema waraka huo unawataka wazazi na walezi kutowatuma watoto kuanzia saa 12.00 jioni. 

“Ni marufuku mtoto kutumwa kuanzia saa 12, wazazi na walezi wanatakiwa kuwalinda na kuwatunza watoto wao kwa kuwahakikishia usalama,” alisema.

Waraka huo pia umezuia watoto kuzurura hovyo mitaani kwa kuwa wabakaji wamekuwa wakitumia mbinu nyingi ikiwamo kuwalaghai kwa pipi au kuwatuma. 

“Ni marufuku watoto kuonekana baa au vilabu vya pombe za kienyeji, ikibainika wamiliki watachukuliwa hatua kali za kisheria,” alisema.

Alisema matatizo ya ubakaji na kuwalawiti watoto yamekuwa sugu na kwamba unahitaji ushirikiano baina ya polisi, wananchi na viongozi kupambana nayo.

“Nimeagiza polisi kuongeza doria na watuhumiwa wanaokamatwa kwa ubakaji, sheria ichukue mkondo wake ili kukomesha hali hii,” alisema.

Aliwaomba viongozi wa dini kusaidia kutoa elimu kwa waumini wao juu ya kuwalinda watoto na kukemea ukatili huo ambao ni hatari ikiwa utaachwa kuendelea.

Naibu Meya wa Manispaa ya Iringa, Joseph Lyata alisema imani za kishirikina zimechangia ubakaji na ulawiti kwa watoto kukithiri.

Alisema katika uchunguzi wao walibaini vikaratasi vilivyokuwa vikisambazwa mitaani vikishauri wanaume wanaotaka kufanikiwa kimaisha, wabake na kulawiti watoto wadogo kisha wajiunge na dini yao ya ‘freemason’.

“Mtaa wa Semtema ndiyo ulikuwa tishio na huko tuliokota vikaratasi vilivyokuwa vimeandikwa ukitaka kutajirika, jiunge na freemason pia ubake au kulawiti mtoto chini ya miaka 14,” alisema.

Lyata alisema sababu nyingine ni ulevi wa kupindukia na utumiaji wa dawa za kulevya kama bangi.

Alisema kukithiri kwa vitendo hivyo kumeifanya manispaa hiyo kutangaza jambo hilo kuwa ni janga ambalo lazima wapambane nalo kwa kuwasaka wabakaji.

Naibu meya aliwataka polisi kudhibiti vitendo hivyo vinginevyo watoto wataendelea kuteseka.

Alisema wapo watoto wanaofanyiwa ukatili huo majumbani na wengine mitaani. Alisema wameanza kuwatambua watoto wa mitaani na kuwarudisha makwao ili kuwanusuru kubakwa. 

Watoto wasimulia 
Baadhi ya watoto walisema wamekuwa wakifanyiwa vitendo hivyo na vijana waliopo mtaani, hasa nyakati za jioni.

 “Siku hiyo nilitumwa na mama dukani, wakati narudi kuna mtu akanipa hela nimnunulie mafuta ya taa nimpelekee kwake, nilipompelekea akanifanyia hivi,” alisema mtoto huyo.

Alisema mbakaji huyo alimtishia endapo atasema angemfanyia tena ukatili huo bila huruma. 

“Nilimpa mama mafuta, nikaenda kulala nikilia sana niliogopa kumwambia, bahati aligundua kwa sababu sikuwa naweza kutembea na aliponikagua akakuta nimeumizwa,” alisema.

Mama wa mtoto huyo alisema mbali na kuumizwa mwanaye aliambukizwa magonjwa ya zinaa. Aliiomba Serikali kutowanyamazia wanaume wenye tabia ya kuwabaka watoto.

Mtoto mwingine wa kiume alisema kijana asiyemjua alimpatia pipi akijifanya rafiki yake, hali iliyomfanya waongozane hadi mlima wa Semtema, ambako alimlawiti. 

Wananchi walia 
Kukithiri kwa vitendo hivyo kuliwafanya wananchi waandamane hadi kwa mkuu wa wilaya kuomba msaada. Wananchi hao walieleza kuwa kinachowatesa ni watuhumiwa kuachiwa huru na polisi na kurejea mtaani.

“Ndiyo maana tumeamua tutakayemkuta tunammaliza kwa sababu akienda polisi atarudi tu,” alisema Gerald Matibabu.

Wazazi hao walidai vitendo hivyo vimewachosha, na kwamba wapo watoto walioambukizwa magonjwa ya zinaa ikiwamo Ukimwi.

Mwenyekiti wa mtaa wa Semtema wenye wakazi 3,800, Reminus Ndale alisema mpaka sasa idadi ya watoto waliofanyiwa unyama huo kwenye mtaa wake ni wanne.

Alisema kwa kushirikiana na wananchi wameamua kuhakikisha watoto wao wanalindwa na kuwachukulia hatua kali watakaobainika kuwabaka.

Polisi wazungumza 
Kaimu Kamanda wa Polisi mkoani Iringa, John Kauga alikiri kuwapo kwa vitendo vya ulawiti na ubakaji na kuwataka wananchi kutoa taarifa haraka vinapotokea.

“Kuna matukio mengi pia majumbani, wazazi wasifiche, watoe taarifa kwa polisi ili hatua kali za kisheria zichukuliwe,” alisema.

Aliwataka wananchi kupinga imani za kishirikina zinazowahamasisha kufanya ukatili kwa watoto kwa madai ya kutajirika


This post first appeared on MASWAYETU, please read the originial post: here

Share the post

Watoto Mkoani Iringa Wapigwa Marufuku Kutembea Saa 12 jioni na Kuendelea

×

Subscribe to Maswayetu

Get updates delivered right to your inbox!

Thank you for your subscription

×