Na Mwantanga Ame
MATAYARISHO ya sikukuu ya Muungano yameanza kukamilika ambapo kwa mwaka huu zitafanyika Makao Makuu ya Tanzania mkoani Dodoma.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais, Mohamed Aboud, aliyasema hayo jana wakati akizungumza na Zanzibar Leo huko Ofisini kwake Vuga Mjini Unguja.
Waziri Aboud alisema, tayari hivi sasa kumekuwa na matayarisho mbali mbali yanayoendelea kufanywa na watendaji waliopewa jukumu la kusimamia shughuli hiyo.
Maadhimisho ya sikukuu hiyo ni mara ya kwanza kusherehekewa katika Mkoa huo, tangu Muungano kuundwa kati ya Tanganyika na Zanzibar.
Maadhimisho hayo yatafanyika ikiwa ni kutimiza miaka 54 ya Muungano, ambapo mara nyingi huadhimishwa katika viwanja vya Taifa Dar es Salaam na Uwanja wa Amani Mjini Unguja.
Aboud, alisema wakati wakitimiza miaka hiyo, tayari serikali ya Zanzibar na Serikali ya Muungano, kumekuwa na mafanikio mbali mbali yaliojitokeza huku zikiendelea kuzishughulikia baadhi ya changamoto zilizobakia.
Kutokana na hilo, Waziri Aboud alisema kuwa serikali itahakikisha inazifanyia kazi changamoto hizo, na ni vyema kwa wananchi kuiunga mkono serikali yao pamoja na kudumisha amani.
Credit: Zanzibarleo