Get Even More Visitors To Your Blog, Upgrade To A Business Listing >>

"Sifukuziki CUF": Maalim Seif





Mgogoro wa uongozi ndani ya Chama cha Wananchi (CUF) unaendelea kukitikisa chama hicho baada ya Katibu Mkuu wake, Maalim Seif Sharif Hamad kusema Profesa Ibrahim Lipumba hana uwezo wa kumfukuza uanachama huku akimwambia, “Sifukuziki.”

Maalim Seif alitoa kauli hiyo Jumamosi, Machi 24, 2018 katika kongamano la kujadili mwenendo wa chama hicho lililofanyika Tandale, mjini Dar es Salaam kumjibu Profesa Lipumba ambaye ni Mwenyekiti wa CUF anayetambuliwa na Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa.

Kauli ya Maalim Seif ambaye ni Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Mstaafu katika Serikali ya Umoja wa Kitaifa (SUK), imekuja baada ya Profesa Lipumba kusema Maalim Seif atajadiliwa na Kamati ya Maadili na Nidhamu ya CUF kwa utovu wa nidhamu na kukidhoofisha chama hicho.

Katika kile kilichoonekana kumjibu Profesa Lipumba, Maalim Seif alisema kamwe hatakwenda kuhojiwa kwenye kamati hiyo aliyodai ni haramu akisema ipo kinyume cha sheria na taratibu za chama hicho.

“Nitabaki kuwa katibu wa chama hiki hadi uchaguzi wa CUF utakapofanyika mwakani. Kamati ya Maadili inamwita Seif…Seif yupi?. Maalim seif alihoji na kuongeza, “Siwezi kuungana na wasaliti hata siku moja na wasijisumbue.”

Alidai kwamba kuna mipango inaratibiwa ya kumfukuza katika wadhifa wake ili nafasi hiyo apewe kiongozi mmoja wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ).

“Kiongozi huyo akiwa Katibu Mkuu, atapata fursa ya kugombea urais wa Zanzibar lakini ninawaeleza kamwe hawawezi kufanikiwa,” alisema Maalim Seif.

Akijibu madai hayo, Mkurugenzi wa Habari na Mawasiliano ya Umma (CUF Lipumba), Abdul Kambaya alisema anachokifanya Katibu Mkuu huyo ni sawa na kupiga ramli akisema kitendo chake cha kutofika ofisi za chama hicho, sawa na kujifukuza.

“Maalim Seif alishajifukuzisha CUF kwa sababu hafiki Ofisini Buguruni. Kwa hiyo hatuwezi kufukuzana na kulumbana na kivuli chetu wenyewe,” alisema Kambaya.

Katika kongamano hilo, Maalim Seif pia aligusia jinsi Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) ulivyompokea aliyekuwa mgombea urais wa CHADEMA katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015, Edward Lowassa na kubainisha kuwa Profesa Lipumba alishiriki kumleta, jambo ambalo mara kadhaa msomi huyo amekuwa akilikanusha.

Pia, Maalim Seif alisema hivi karibuni atafanya ziara kisiwani Pemba na kusema anataka kujihakikishia kama kweli Profesa Lipumba ana wafuasi wengi kisiwani humo kama alivyodai baada ya ziara yake mwezi uliopita.

“Ninawataka wanachama wa CUF kuendelea na mshikamano maana haki itapatikana. Mjitokeze kwa wingi katika kesi zinazoendelea mahakamani…Tuamini kuwa haki itatendeka,” alisema Maalim Seif.

Kongamano hilo lilihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa CUF (upande wa Maalim Seif), akiwemo mkurugenzi wa uchaguzi, Sheweji Mketo na Naibu Katibu Mkuu, Joran Bashange na madiwani.

Katika kikao cha Baraza la Uongozi kilichofanyika Machi 22, Profesa Lipumba alidai kuwa Maalim Seif…ameidhoofisha CUF kwa kuwakumbatia viongozi wa CHADEMA.

Kadhalika, Lipumba alimlaumu Maalim Seif kwa kutotekeleza azimio la Baraza Kuu la kufungua kesi Mahakama Kuu ya Zanzibar kupinga kufutwa kwa matokeo ya uchaguzi wa wawakilishi na madiwani ambao alisema walikabidhiwa hati za ushindi wa majimbo na shehia zao katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015.


This post first appeared on Maisha Yetu, please read the originial post: here

Share the post

"Sifukuziki CUF": Maalim Seif

×

Subscribe to Maisha Yetu

Get updates delivered right to your inbox!

Thank you for your subscription

×