Get Even More Visitors To Your Blog, Upgrade To A Business Listing >>

GGML YATOA MILIONI 150 KUDHAMINI MAONESHO YA 6 YA TEKNOLOJIA YA MADINI GEITA


Mkurugenzi Mtendaji wa GGML, Terry Strong (kulia) akipata maelezo kutoka kwa mmoja wa wafanyakazi wa kitengo cha huduma za dharura cha kampuni hiyo pindi waliposhiriki Maonesho Hayo mwaka jana. Kushoto ni Makamu Rais wa AngloGold Ashanti- GGML anayesimamia miradi endelevu kwa upande wa Ghana na Tanzania, Simon Shayo

Na Mwandishi Wetu 

KATIKA kuendelea kudumisha dhamira ya ubunifu wa kiteknolojia, Kampuni ya Geita Gold Mining Limited (GGML) imetoa kiasi cha Sh milioni 150 kudhamini Maonyesho ya Sita ya Teknolojia ya Madini yanayofayika mkoani Geita.

Maonyesho hayo ambayo hufanyika kila mwaka, mwaka huu yanatarajiwa kuzinduliwa tarehe 23 na kuhitimishwa tarehe 30 Septemba.

Maonyesho hayo yanafanyika kwa ushirikiano kati ya Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Geita na Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TANTRADE), katika viwanja vya Bombambili vilivyopo eneo la Mamlaka ya Maeneo ya Usindikaji Nje (EPZA) mkoani humo.

Akizungumzia ushiriki wa GGML katika Maonesho hayo mjini Geita jana, Meneja Mwandamizi wa kampuni hiyo anayesimamia mahusiano jamii, Gilbert Mworia alisema maonesho hayo yamekuwa na mvuto wa kipekee tangu yalipoasisiwa kutokana na ufadhili wa GGML kupitia mfuko wa uwajibikaji kwa jamii (CSR) ambao uliwezesha ujenzi wa eneo hilo la EPZA pamoja na eneo la uwanja huo wa maonesho.

"Mbali na maonyesho, tuliwekeza Sh 800 milioni katika ujenzi wa jengo la utawala la EPZA. Tunafurahi kuona mpango wetu wa EPZA mkoani Geita unastawi na kutimiza malengo ya jamii ya wana-Geita kikamilifu," alisema na kuongeza;

"Msaada wetu unavuka usaidizi wa kifedha ambao tumeendelea kuutoa kila mwaka, kwa sababu tulitoa msaada wa maandalizi ya maonesho hayo kama vile mahema, jenereta la dharura na mafuta yanakayotumika kwa wakati wote wa maonesho,” alisema Mworia.

Alisema katika kipindi cha miaka sita ya ushirikiano huo na wadau wa maonesho hayo, GGML imeendelea kuelimisha jamii kuhusu teknolojia inayotumika katika vifaa vya uchimbaji madini hali inayoendelea kukuza uhusiano imara kati yake, kampuni za ndani na wachimbaji madini.

Aidha, alisema ili kutimiza malengo ya muda mrefu ya ukuaji wa uchumi endelevu, GGML inaunga mkono Dira ya 2025 ya serikali. Mpango huu unalenga kuiwezesha sekta ya uchimbaji madini kukua na kufikia kiwango cha asilimia 10 kwenye Pato la Taifa la Tanzania.

Ufunguzi rasmi wa Maonesho hayo ya 6 ya Madini na Teknolojia mkoani Geita utafanywa na Dk. Dotto Biteko, Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, tarehe 23 Septemba.

Tarehe 30 Septemba mwaka huu, Rais Samia Suluhu Hassan anayetarajiwa kufunga maonesho hayo yenye kauli mbiu; Matumizi ya teknolojia sahihi katika kuinua wachimbaji wadogo kiuchumi na kuhifadhi mazingira.






This post first appeared on MASWAYETU, please read the originial post: here

Share the post

GGML YATOA MILIONI 150 KUDHAMINI MAONESHO YA 6 YA TEKNOLOJIA YA MADINI GEITA

×

Subscribe to Maswayetu

Get updates delivered right to your inbox!

Thank you for your subscription

×