Get Even More Visitors To Your Blog, Upgrade To A Business Listing >>

NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI AITAKA TRC KUONGEZA KASI KATIKA KUSIMAMIA MIRADI INAYOENDELEA ILI IKAMILIKE KWA WAKATI NA KWA THAMANI HALISI YA FEDHA

Ziara ya Naibu Waziri wa Uchukuzi Mhe. David Kihenzile ya kutembelea Uongozi wa Shirika la Reli Tanzania(TRC) Kwa ajili ya kujitambulisha, kujifunza na kujionea miradi inayoendelea chini ya Usimamizi wa Shirika Hilo na kukagua Stesheni ya treni ya kisasa ya SGR ya Tanzanite Jijini Dar es salaam

Na Mwandishi wetu Dar es Salaama 

Naibu Waziri wa Uchukuzi Mhe David Kihenzile ameutaka uongozi wa Shirika la Reli Tanzania(TRC) kuongeza kasi katika kusimamia miradi inayoendelea ili Ikamilike Kwa Wakati na kwa thamani halisi ya fedha.


Mhe kahenzile ameyasema hayo wakati wa ziara ya kujitambulisha, kujifunza , kuongea na Menejimenti ya Shirika na kujionea miradi inayotekelezwa na kusimamiwa na shirika la reli Tanzania kwenye ofisi za shirika hilo zilizopo stesheni Jijini Dar es salaam tarehe 13 Septemba,2023.


“Naupongeza uongozi wa Shirika kwa usimamizi makini wa miradi inayoendelea ya uboreshwaji wa reli ya kati na ujenzi wa Reli ya kisasa(SGR) ,ununuzi wa mabehewa na vichwa vya treni, Miradi hii kwa sasa ni jicho la nchi yetu hivyo natoa rai kwenu muongeze kasi ya usimamizi ili ikamilike kwa wakati na thamani halisi ya fedha kwani tunaitegemea sana ili kuinua uchumi wa wananchi, sekta zingine, kuongeza mapato ya shirika na hatimaye muweze kujitegemea na kujiendesha”amesisitiza Mhe Kihenzile



Mhe Kihenzile amemshukuru Rais wa awamu ya sita Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kumuamini na kumteua kwa nafasi ya Naibu Waziri Uchukuzi ili amsaidie Waziri Prof Makame Mbarawa na kuahidi ushirikiano wa karibu wa Wizara ya Uchukuzi na Taasisi zake zote ili kuongeza kasi ya utendaji na hatimaye kuongeza tija kwa Taifa.


Akitoa salamu za Shirika Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Reli Tanzania Bi. Amina Lumuli amesema shirika hilo liliundwa mwaka 2017 baada ya kuvunjika kwa RAHCO na TRL na kurithi majukumu yaliyokuwa yakitekelezwa na mashirika hayo ikiwemo kuanzisha,kusimamia,kuendeleza miundombinu ya Reli, kutoa huduma,kufanya ukarabati,kuingia mikataba na kuimarisha vitendea kazi kulingana na sheria ya reli namba kumi ya Mwaka 2017.



Bi Amina amesema mtandao wa reli Nchini umegawanyika katika kanda tatu ikiwemo reli ya kati(DSM-KGM), reli ya kaskazini(TAN-MOS-ARU), na reli ya kusini(Mtwara-Mbamba bay), huku kukiwa na aina mbili za reli ya kawaida(MGR) yenye urefu wa km 2,707 na reli mpya ya kisasa(SGR) ambapo km 4,752 zinatarajiwa kujengwa.


Kuhusu Miradi inayoendelea Bi Amina amesema Shirika lilipata mkopo wa Dola za Kimarekani Milioni 300 kutoka Benki ya Dunia mwezi machi,2014 kwa ajili ya kuendeleza na kuboresha mradi wa usafirishaji wa reli kutoka tani 135 km ekseli hadi tani 18.5, uboreshaji madaraja na ununuzi wa mabehewa 44 ya mizigo ambavyo vimeshakamilika



Kwa upande wa Reli ya Mwendokasi(SGR) Bi Amina amesema ujenzi wa reli kutoka DSM hadi Mwanza wenye jumla ya km 1,596 unaohusisha km 1,219 njia kuu na km 377 za mapishano umefikia katika hatua mbalimbali za utekelezwaji zilizogawanywa kwa vipande vitano kwa awamu ya kwanza ambavyo ni Dsm-Moro(km300) asilimia 98.52, Moro-Makutupora(km422) asilimia 94.99, Makutupora-Tabora(km368) asilimia 10.92, Tabora-Isaka(km 165) asilimia 4.63 na Isaka-Mwanza (km 341) asilimia 37.22.


“Ujenzi wa reli ya kisasa unaendelea vizuri awamu ya kwanza na kwa awamu ya pili ya kipande cha Tabora-kigoma(km 506) usanifu unaendelea ambapo mpaka sasa jumla ya Dola za kimarekani Bil 3.75 sawa na Zaidi ya shilingi tril 23 zimeshatumika na tayari jumla ya vichwa vya treni vya umeme 17 na seti 10 za EMU ukarabati unaendelea Nchini korea,mabehewa ya mizigo 1,430 yameagizwa na tayari mabehewa ya abiria 59 yalishawasili” amesisitiza Bi Amina


Mnamo tarehe 30 Agosti,2023 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt Samia Suluhu Hassan alifanya mabadiliko madogo ya baraza la mawazili na makatibu wakuu yaliyopelekea kuanzishwa kwa Wizara mpya ya Uchukuzi na kuteuliwa Prof Makame mbarawa kuwa Waziri, Mhe David Kihenzile Naibu Waziri, Prof Godius Kahyarara katibu mkuu na Dkt Ally Possi Naibu katibu Mkuu.





This post first appeared on MASWAYETU, please read the originial post: here

Share the post

NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI AITAKA TRC KUONGEZA KASI KATIKA KUSIMAMIA MIRADI INAYOENDELEA ILI IKAMILIKE KWA WAKATI NA KWA THAMANI HALISI YA FEDHA

×

Subscribe to Maswayetu

Get updates delivered right to your inbox!

Thank you for your subscription

×