Get Even More Visitors To Your Blog, Upgrade To A Business Listing >>

SERIKALI WADAU WAIPONGEZA BENKI YA CRDB KUKUSANYA SH 700 BILIONI KUWAWEZESHA WAJASIRIAMALI NCHINI


Waziri wa Uchumi wa Buluu na Uvuvi wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ), Abdalla Hussein Kombo (katikati), Afisa Biashara Mkuu Benki ya CRDB, Boma Raballa (wapili kushoto), Mkurugenzi wa Wateja Wadogo na Wakati Benki ya CRDB, Bonaventura Paul (wapili kulia), Mkuu wa Kitengo cha Huduma kwa Wateja Benki ya CRDB, Yolanda Uriyo (wakwanza kushoto), na Meneja Mwandamizi Kitengo cha Biashara, Agnes Kisinini wakiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya wateja wajasiriamali wa Benki hiyo wakati wa hafla maalum ya kuadhimisha Siku ya Wajasiriamali Duniani iliyoandaliwa iliyofanyika 27 Juni 2023 Makao Makuu ya Benki ya CRDB jijini Dar es Salaam.

====== ===== =====


Serikali imeipongeza Benki ya CRDB kwa kukusanya zaidi ya Sh700 bilioni za kuwakopesha wafanyabiashara wadogo na wa kati nchini katika maadhimisho ya Siku ya Wajasiriamali Duniani (World MSME Day).


Pongezi hizo zimetolewa na Waziri wa Uchumi wa Buluu na Uvuvi wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ), Abdalla Hussein Kombo aliyekuwa mgeni rasmi kwenye maadhimisho hayo akisema jitihada zinazofanywa na Benki hiyo zinaonyesha dhamira ya dhati iliyonayo katika kuchochea sekta ya ujasiriamali nchini.


“Takwimu zinaonyesha ni asilimia 96 ya biashara nchini ni biashara ndogo na za kati, ambapo watu milioni 24 wameajiriwa katika sekta hii. Hivyo jitihada hizi zinazofanywa na Benki ya CRDB ni muhimu sana katika kuboresha sekta hii ambayo inatoa mchango mkubwa katika ukuaji wa uchumi wa Taifa letu,” amesema Kombo.
Waziri Kombo amebainisha kuwa, sekta ya ujasiriamali inachangia asilimia 33 kwenye pato la Taifa yaani Gross Domestic Product (GDP). Hii ikimaanisha kuwa, katika kila shilingi 100 basi shilingi 33 ambazo ni sawa na theluthi moja, zinachangiwa na biashara ndogo.


Benki ya CRDB inatajwa kuwa kinara katika uwezeshaji wa wajasiriamali nchini huku mwaka huu ikitunikiwa tuzo ya Benki Bora kwa uwezeshaji wa Wajasiriamali na jarida maarafu la nchini marekani la “Global Finance”.
Kwa upande wa Zanzibar, Waziri Kombo amesema Serikali inajivunia ushirikiano na Benki ya CRDB kupitia programu ya “INUKA NA UCHUMI WA BLUU” kuwainua wajasiriamaili ambapo shilingi bilioni 60 zimetengwa.


Programu hiyo ambayo inatoa ufadhili wa mitaji kwa wajasiriamali bila riba inatajwa kuwa moja ya programu bunifu zenye msukumo mkubwa wa kuwainua wajasiriamali nchini. “Wizara yangu ni miongoni mwa sekta zilizonufaika na mikopo inayotolewa na Benki ya CRDB kupitia programu ya INUKA kwani imetengewa Sh36.5 bilioni kila mwaka kwa ajili ya kuwawezesha wajasiriamali wadogo wanaojihusisha na fursa zilizopo kwenye uchumi wa buluu. Kwa kweli naipongeza sana Benki ya CRDB kwa juhudi hizi muhimu kwa uchumi wa Taifa na maendeleo ya watu wetu,” amesema Waziri Kombo.

Kwa upande wake, Afisa Mkuu wa Biashara wa Benki ya CRDB, Boma Raballa Benki ya CRDB inatambua na kuthamini shughuli za kijasiriamali katika kusukuma gurudumu la maendeleo ya wananchi na taifa kwa ujumla jambo ambalo limeifanya benki hiyo kushirikiana na wadau mbalimbali ndani na nje ya nchi katika kuboresha sekta hiyo.


“Katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita wakati dunia ikishuhudia misukosuko ya kiuchumi iliyochangiwa na janga la UVIKO-19 na vita vya Ukraine, Benki yetu kwa kushirikiana na washirika wa kimataifa ilikusanya zaidi ya Sh 700 bilioni ambazo zinaendelea kusaidia biashara za wajasiriamali ambazo nyingi ziliziathirika kwa kiasi kikubwa,” amesema Raballa.
Katika kipindi hicho, Raballa amesema wameshirikiana na wadau wa ndani na kimataifa likiwamo Shirika la Fedha la Ufaransa Proparco, Shirika la Fedha Kimataifa (IFC), Mashirika ya Marekani ya Maendeleo ya Kimataifa USAID na DFC, Benki ya Uwekezaji ya Umoja wa Ulaya, Benki ya Maendeleo Afrika (AfDB), na Mfuko wa Dhamana Afrika (AGF) kukusanya kiasi hicho cha fedha.


Raballa amesema ili sekta ya ujasiriamali iweze kutoa mchango wake kikamilifu katika kukuza uchumi wa Taifa, kunahitajika huduma na mifumo shirikishi itakayowasaidia wajasiriamali kufanikisha malengo yao.


Kwa kutambua hilo, Benki ya CRDB ilikuwa benki ya kwanza nchini kuanzisha huduma kwa ajili ya wajasiriamali mwaka 2005 ambapo tokea kipindi hicho imekuwa ikiwekeza kwa kiasi kikubwa katika bidhaa na huduma bunifu za wajasiriamli.


Huduma na bidhaa hizo zinajumuisha akaunti maalumu ya Hodari ambayo ni mahsusi kwa ajili ya wajasiriamali, mifumo ya kidijitali ya usimamizi wa biashara, mafunzo ya ujasiriamali ndani na nje ya nchi, na kutoa mikopo ya mtaji kwa wajasiriamali walio katika sekta tofauti za uchumi.


“Najivunia kuwajulisha kuwa kupitia jitihada hizi, Benki yetu imekuwa kinara katika kuwawezesha wajasiriamali kwani hadi Mei 2023 tulikuwa tumetoa mikopo yenye thamani ya zaidi ya Sh3.4 trilioni kwa wajasiriamali zaidi ya 200,000, na wengine zaidi ya 50,000 wakinufaika kwa mafunzo tuliyoyatoa,” amesema Raballa.


Raballa amesema hivi karibuni Benki ya CRDB kupitia Taasisi yake ya CRDB Bank Foundation imeendelea kupanua wigo wa kuwainua wajasiriamali wadogo kupitia programu endelevu ya “IMBEJU” inayolenga kufanya uwezeshaji wa biashara changa na wajasiriamali vijana na wanawake kupitia mafunzo, ushauri, na mitaji wezeshi.

Akizungumza kwenye mjadala wa maadhimisho hayo, Mkurugenzi Mtendaji wa Chama cha Wanawake Wafanyabiashara Tanzania (TWCC), Mwajuma Hamza ameipongeza Benki ya CRDB kwa kuwa mdau mkubwa wa sekta ya ujasiriamali hususan kwa kuweka mbele uwezeshaji wa wajasiriamali wanawake kupitia CRDB Malkia inayojumuisha Akaunti ya Malkia na Mikopo maalum ya kinamama ijulikanayo kama WAFI (Women Access to Finance Initiatives), huku akibainisha wanawake wajasiriamali wengi wameweza kunufaika na Sh 700 bilioni zilizokusanywa na Benki ya CRDB kusaidia wajasiriamali baada ya changamoto za janga la UVIKO-19.


“TWCC ni chama chenye matawi kila wilaya nchini. Tunashirikiana na wadau kusaidia kutatua changamoto zilizopo. Benki ya CRDB ni miongoni mwa wadau wetu muhimu kwani, licha ya kutukopesha ili nasi tuwawezeshe wanachama wetu, wao ni walezi wazuri. Benki ya CRDB inazo programu nyingi zinazomlenga mwanamke ambaye akizitumia fursa hizo inakuwa rahisi kwake kuboresha biashara yake," amesema Mwajuma.






This post first appeared on MASWAYETU, please read the originial post: here

Share the post

SERIKALI WADAU WAIPONGEZA BENKI YA CRDB KUKUSANYA SH 700 BILIONI KUWAWEZESHA WAJASIRIAMALI NCHINI

×

Subscribe to Maswayetu

Get updates delivered right to your inbox!

Thank you for your subscription

×