Get Even More Visitors To Your Blog, Upgrade To A Business Listing >>

WAKAGUZI WA NDANI WATAKIWA KUTOA USHAURI WENYE TIJA KWA SERIKALI KATIKA MIRADI NA MIFUMO YA TEHAMA

Mkaguzi Mkuu wa Ndani Msaidizi wa Hesabu za Serikali Bw. Paison Mwamnyasi akizungumza wakati wa mafunzo maalum kwa Wakaguzi wa Ndani
Mkurugenzi wa Udhibiti na Usalama wa TEHAMA Mamlaka ya Serikali Mtandao (e-GA) Bw. Sylvani Shayo akizungumza wakati wa mafunzo maalum kwa Wakaguzi wa Ndani
Washiriki wa mafunzo wakiwa ukumbini 

****
Mkaguzi Mkuu wa Ndani Msaidizi wa Hesabu za Serikali Bw. Paison Mwamnyasi, amewataka Wakaguzi wa Ndani kuzingatia sheria, kanuni, viwango na miongozo ya Serikali Mtandao wanapofanya ukaguzi kwenye miradi na Mifumo ya TEHAMA, ili waweze kutoa ushauri wenye tija kwa serikali kupitia taarifa zao za ukaguzi.

Bw. Mwamnyasi aliyasema hayo hivi karibuni wakati wa ufunguzi wa awamu ya pili ya mafunzo maalum kwa Wakaguzi wa Ndani kutoka halmashauri na Tawala za Mikoa 13 za Tanzania Bara.

Alisema kuwa, mafunzo ya ukaguzi wa mifumo na miradi ya TEHAMA Serikalini ni muhimu kwa Wakaguzi wa Ndani kwa kuwa yanawajengea uwezo katika utendaji kazi na kurahisisha shughuli za ukaguzi sambamba na kutoa ushauri wenye tija kwa serikali.

“Ukielewa namna mifumo inavyofanya kazi, unaweza kukagua ipasavyo, na tutaepuka kutaja majina ya watu katika taarifa zetu za ukaguzi badala ya mifumo, sisi Wakaguzi tunatambua kuwa miongozo ya ukaguzi inaeleza kutokagua sehemu ambayo hauna uelewa nayo kwa kuwa unaweza kutoa maoni na ushauri kwa Serikali ambao hauna tija” aliongeza.

Aidha, Mkurugenzi wa Udhibiti na Usalama wa TEHAMA Mamlaka ya Serikali Mtandao (e-GA) Bw. Sylvani Shayo, aliwasisitiza Wakaguzi wa Ndani kutumia Sheria, Kanuni, Viwango na Miongozo ya Serikali Mtandao wakati wa kusimamia na kufanya ukaguzi wa miradi na mifumo ya TEHAMA katika taasisi zao.

Alibainisha kuwa, e-GA kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkaguzi Mkuu wa Ndani wanaendelea na jitihada za kutoa mafunzo kwa Wakaguzi wa Ndani ili waweze kufanya ukaguzi katika eneo la TEHAMA kwa ufanisi.

“Sheria, Kanuni, Viwango na Miongozo ya Serikali Mtandao ni nyenzo muhimu katika ukaguzi wa miradi na mifumo ya TEHAMA katika taasisi za umma, na ikiwa wakaguzi wa ndani mtazingatia vema miongozo na sheria hizo mtafanya ukaguzi wenye tija na maslahi kwa taifa”, alisema Bw. Shayo.

Naye Meneja wa Udhibiti wa Viwango na Miongozo ya Serikali Mtandao Bi. Sultana Seiff alisema, e-GA haitaki kuacha kada yoyote nyuma katika matumizi ya TEHAMA kwakuwa dunia ya sasa inaendeshwa kidijitali, hivyo wakaguzi wa ndani wanapewa mafunzo hayo ili kuongeza ufanisi katika utendaji kazi na kuboresha utoaji wa huduma za Serikali kwa njia ya kidijitali.

Mafunzo hayo ya siku tano yanayofanyika mkoani Morogoro yameanza Juni 05 mwaka huu yanahusisha wakaguzi wa ndani 110 kutoka Halmashauri na Tawala za Mikoa ya Dodoma, Tabora, Singida, Kigoma, Mara, Dar es Salaam, Morogoro, Shinyanga, Rukwa, Kagera, Geita, Simiyu na Katavi. Awamu ya kwanza ya mafunzo hayo yalifanyika Machi mwaka huu ambapo jumla ya Wakaguzi wa Ndani 133 kutoka Halmashauri na Tawala za Mikoa 13 za Tanzania Bara, walishiriki.


This post first appeared on MASWAYETU, please read the originial post: here

Share the post

WAKAGUZI WA NDANI WATAKIWA KUTOA USHAURI WENYE TIJA KWA SERIKALI KATIKA MIRADI NA MIFUMO YA TEHAMA

×

Subscribe to Maswayetu

Get updates delivered right to your inbox!

Thank you for your subscription

×