Get Even More Visitors To Your Blog, Upgrade To A Business Listing >>

HISTORIA YA MALKIA ELIZABETH II WA UINGEREZA

CHANZO CHA PICHA,CHRIS LEVINE/ JERSEY HERITAGE TRUST

Maelezo ya picha,

Malkia Elizabeth II

Utawala wa muda mrefu wa Malkia Elizabeth II ulijawa na hisia kuu za kuwajibika na kujitolea kwake maisha yake yote kwa cheo chake kama malkia na pia kwa watu wake.

Kwa watu wengi, yeye alikuwa kitu kimoja ambacho hakikubadilika ulimwengu ulipokuwa unabadilika kwa kasi na nguvu za Uingereza duniani kupungua. Jamii ilibadilika pakubwa na majukumu na manufaa ya familia ya kifalme nayo yakaanza kutiliwa shaka.

Kufanikiwa kwake Katika kudumisha pamoja familia ya kifalme katika kipindi hicho cha misukosuko kulikuwa jambo kubwa sana, hasa ikizingatiwa kwamba wakati wa kuzaliwa kwake, hakuna aliyetarajia kwamba angeishia kuwa malkia, na kwa muda mrefu.

Elizabeth Alexandra Mary Windsor alizaliwa mnamo 21 Aprili 1926, katika jumba lililokuwa karibu na Berkeley Square jijini London.

Alikuwa kifungua mimba wa Albert, Mwanamfalme Mtawala wa York, aliyekuwa mwana wa pili wa kiume wa George V, na mkewe ambaye zamani alifahamika kama Lady Elizabeth Bowes-Lyon.

CHANZO CHA PICHA,GETTY IMAGES

Maelezo ya picha,

Elizabeth akiwa na wazazi wake wakati wa kubatizwa

Elizabeth na dadake, Margaret Rose, aliyezaliwa mwaka 1930, walipewa elimu nyumbani na kulelewa katika mazingira ya familia yaliyojaa upendo.

Elizabeth alikuwa na uhusiano wa karibu sana na babake na babu yake, George V.

Alipokuwa na miaka sita, Elizabeth alimwambia mwalimu wake wa uendeshaji farasi kwamba alitaka kuwa "mwanamke wa kukaa mashambani na awe na farasi na mbwa wengi."

Alidaiwa kuanza kuonyesha hisia za juu sana za kuwajibika kutoka akiwa na umri mdogo sana.

Winston Churchill, ambaye baadaye alikuwa waziri mkuu, alinukuliwa akisema kwamba "alionyesha hisia za kuwa na mamlaka, ambazo zilikuwa nadra sana kupata kwa mtoto kama yeye."

Licha ya kutohudhuria masomo katika shule ya kawaida, Elizabeth alifanya vyema sana katika kuzifahamu lugha mbalimbali na alifanya usomaji wa kina wa historia ya kikatiba.

Kundi maalum la maskauti wa kike, maarufu kama Girl Guides, lililofahamika kama 1st Buckingham Palace liliundwa ili aweze kujumuika na kuzoeana na wasichana wa rika lake.

Maelezo ya picha,

Bintimfalme Elizabeth (kulia) na Margaret wakitangaza kwenye kipindi cha redio wakati wa Vita Vikuu vya Pili vya Dunia

Kuongezeka kwa wasiwasi

CHANZO CHA PICHA,GETTY IMAGES

Maelezo ya picha,

Princess Elizabeth, akiwa na wazazi wake na dadake mdogo Margaret, wakati wa kutawazwa kwa babake kuwa mfalme, sherehe ambayo ilikuwa "ya kuvutia na ya kufana sana".

Baada ya kifo cha George V mwaka 1936, mwanawe mkubwa wa kiume, aliyefahamika kama David, alirithi ufalme na kuwa Mfalme Edward VIII.

Hata hivyo, mwanamke aliyeamua kumuoa, Mmarekani aliyekuwa ametalikiwa mara mbili Wallis Simpson, hakukubalika kwa misingi ya kisiasa na kidini wakati huo. Mwishoni mwa mwaka, alijiuzulu.

Mwanamfalme Mtawala wa York, babake Malkia Elizabeth, alichukua ufalme na kuwa Mfalme George VI. Kutawazwa kwake kulimdokezea Elizabeth maisha yaliyomsubiri na baadaye aliandika kwamba aliiona sherehe hiyo kuwa "ya kupendeza sana".

Huku uhasama na wasiwasi ukiongezeka Ulaya, Mfalme huyo mpya, pamoja na mkewe, Malkia Elizabeth, walichukua jukumu la kurejesha imani ya umma katika familia ya kifalme.

Mfano wao ulimgusa binti wao mkubwa.

Mwaka 1939, bintimfalme huyo aliyekuwa na miaka 13 wakati huo, aliandamana na Mfalme na Malkia kwenye hafla katika chuo cha jeshi la wanamaji la Royal Naval College, Dartmouth.

Kwa pamoja na dadake Margaret, alimsindikiza mmoja wa waliokuwa wanafuzu, binamu wake wa kiwango cha tatu, Mwanamfalme Philip wa Ugiriki.

Vikwazo

CHANZO CHA PICHA,PA

Maelezo ya picha,

Harusi ya Bintimfalme Elizabeth na Philip Mountbatten ilirejesha furaha katika mazingira magumu ya baada ya vita

Hiyo haikuwa mara yao ya kwanza kukutana, lakini ilikuwa mara ya kwanza kwake kuanza kuvutiwa naye.

Prince Philip aliwatembelea jamaa zake wa familia ya kifalme alipokuwa likizoni kutoka kwenye jeshi la wanamaji - na kufikia mwaka 1944, alipokuwa na miaka 18, ilikuwa wazi kwamba Elizabeth alikuwa anampenda.

Alikuwa akiweka picha yake katika chumba chake, na walikuwa wakiandikiana pia barua.

Bintimfalme huyo alijiunga na kikosi cha wafanyakazi wa ziada wasaidizi wa jeshi kwa jina Auxiliary Territorial Service (ATS) mwishoni mwa vita, ambapo alijifunza kuendesha na kukarabati lori.

Siku ya kumalizika kwa vita, ambayo hufahamika kama VE Day, alijiunga na jamaa wengine wa familia ya kifalme katika Buckingham Palace huku maelfu ya watu wakikusanyika katika barabara kuu ya kuelekea kasri hilo ambayo hufahamika kama The Mall kusherehekea kumalizika kwa vita Ulaya.

"Tuliwaomba ruhusa wazazi wetu tutoke nje kwenda kujionea wenyewe," alikumbuka baadaye.

"Nakumbuka tulikuwa na wasiwasi sana kwamba tungetambuliwa (na watu). Nakumbuka milolongo mirefu ya watu tusiowafahamu wakishikana mikono na kutembea kuelekea Whitehall, sote tulijumuika nao na kutembea kama waliobebwa na wimbi la furaha na kupata nafuu."

Baada ya vita, nia yake ya kutaka kuolewa na Prince Philip ilikabiliwa na changamoto kadha.

Mfalme hakutaka kumpoteza binti wake ambaye alimpenda sana na Philip alihitajika kuondoa pingamizi la ubaguzi katika familia ya kifalme ambayo haikuwapendelea watu wenye asili ya nje ya nchi.

Kifo cha babake

Lakini matamanio ya wawili hao yalitimia na mnamo 20 Novemba 1947, walifunga ndoa katika kanisa la Westminster Abbey

Mtawala wa Edinburgh, cheo kipya cha Philip, alisalia kuwa mhudumu katika jeshi la wanamaji.

Kwa muda mfupi, alitumwa kuhudumu jeshini Malta, na huko kwa kiasi fulani walifurahia maisha ya kawaida.

Mtoto wao wa kwanza, Charles, alizaliwa 1948, akifuatwa na dadake, Anne, aliyezaliwa 1950.

Lakini Mfalme, baada ya kupata mfadhaiko sana na shinikizo wakati wa vita, alikuwa amezidiwa na ugonjwa wa saratani ya mapafu, ambao ulitokana na kuwa mvutaji sigara sugu.

Januari 1952, Elizabeth, aliyekuwa na miaka 25 wakati huo, akiwa na Philip, walifunga safari ng'ambo.

Mfalme alikaidi ushauri wa madaktari na kwenda uwanja wa ndege kuwaaga.

Ilikuwa ni mara ya mwisho kwa Elizabeth kumuona babake akiwa hai.

Elizabeth alipata habari za kifo cha Mfalme akiwa katika mgahawa wa kitalii katika mbuga moja nchini Kenya na mara moja alirejea London akiwa sasa ndiye Malkia.

Baadaye alikumbuka yaliyotokea.



This post first appeared on MASWAYETU, please read the originial post: here

Share the post

HISTORIA YA MALKIA ELIZABETH II WA UINGEREZA

×

Subscribe to Maswayetu

Get updates delivered right to your inbox!

Thank you for your subscription

×