Get Even More Visitors To Your Blog, Upgrade To A Business Listing >>

Serikali Yakutana Na Taasisi,mashirika Na Mabalozi Kujadili Mapato Na Matumizi Ya Bajeti


 Na Mwandishi wetu
Katika kukuza Diplomasia ya Uchumi, kuimarisha na kushirikisha Jumuiya za Kimataifa Serikali imekutana na Mabalozi, Wakuu na Wawakilishi wa Mashirika na Taasisi za Kimataifa zilizopo hapa nchini kujadili Mapato na Matumizi ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2021/22 pamoja na mbinu za pamoja za kupambana na ugonjwa wa UVIKO 19.

Mkutano huo umefanyika Dar es Salaam na kuhudhuriwa na Wizara za Kisekta zikiwemo Fedha na Mipango, Viwanda na Biashara, Afya, Maliasili na Utalii, Uwekezaji na Wizara ya Fedha na Mipango – Zanzibar pamoja na Mabalozi na Wawakilishi wa mashirika ya Kimataifa 54 kutoka nchi na taasisi mbalimbali.

Lengo la Mkutano huo pamoja na mambo mengine, ni kuwapitisha Mabalozi na Wawakilishi wa Mashirika ya Kimataifa kwenye Bajeti ya Serikali ya 2021/22, Mipango ya Utekelezaji wake na Maeneo ya Ushirikiano.

Akiongoza Mkutano huo Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Liberata Mulamula (Mb) ametaja sababu za Serikali kukutana na Mabalozi pamoja na Wawakilishi wa Mashirika na Taasisi za Kimataifa ambao pia ni wadau wa maendeleo ili kuwajengea uelewa katika mipango na utekelezaji wa Bajeti ya Serikali ya 2021/22 pamoja na maeneo ya Ushirikiano.

“……………………tumeona tuweke utaratibu wa kukutana na wadau hawa wa maendeleo ili kujenga uelewa wa pamoja katika maeneo muhimu yaliyoainishwa katika bajeti ya Serikali ili waweze kupata picha halisi ya mipango na mikakati ya Serikali katika utekelezaji wa Bajeti,” amesema Balozi Mulamula

Kwa Upande wake Balozi wa nchi za Umoja wa Ulaya (EU) hapa Nchini, Mhe. Manfredo Fanti amesema uamuzi wa Serikali wa kukutana na Mabalozi na Wawakilishi wa Mashirika na Taasisi za Kimataifa umekuwa mzuri sana umesaidia kufahamu mipango na mikakati mbalimbali ya Serikali katika utekelezaji wa bajeti yake ya 2021/22.

“Kupitia mkutano wa leo tumeweza kupata picha halisi ya ushirikiano wetu na Tanzania na umezidi kuimarika lakini pia tumeweza kuona na kujadili baadhi ya vipaumbele vya bajeti ya Serikali ya Tanzania, mipango ya maendeleo jambo ambalo sisi kama wadau wa maendeleo limetuhamasisha kuendelea kushirikiana kwa ukaribu n a uwazi zaidi,” amesema Balozi Fanti   

Mkutano huo umehudhuriwa na Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Mwigula Nchema (Mb), Waziri wa Viwanda na Biashara, Prof. Kitila Mkumbo (Mb), Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Damas Ndumbaro (Mb), Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii Jinsia, Wazee na Watoto, Dkt. Dorothy Gwajima (Mb), Waziri wa Fedha na Mipango kutoka Serikalini ya Mapinduzi ya Zanzibar, Mhe. Jamal Kassim Ali, Pamoja na Naibu Waziri Wizara ya Uwekezaji Mhe. William Tate Olenasha (Mb).  

Pamoja na Mambo mengine, Mawaziri hao wamepata fursa ya kutoa ufafanuzi katika maeneo yanayohusu wizara zao ikiwa ni pamoja na mipango ya Serikali katika kukuza uchumi, kukusanya mapato, kukuza Viwanda, kuboresha mazingira ya Biashara na Uwekezaji, kukuza utalii na jinsi Serikali inavyojipanga kuboresha sekta ya afya nchini hasa katika kupambana na janga la UVIKO 19.




This post first appeared on MASWAYETU, please read the originial post: here

Share the post

Serikali Yakutana Na Taasisi,mashirika Na Mabalozi Kujadili Mapato Na Matumizi Ya Bajeti

×

Subscribe to Maswayetu

Get updates delivered right to your inbox!

Thank you for your subscription

×