Get Even More Visitors To Your Blog, Upgrade To A Business Listing >>

Taarifa Ya Hali Ya Uchumi Wa Taifa Kwa Mwaka 2019 Na Mpango Wa Maendeleo Wa Taifa Wa Mwaka 2020/21 Wawasilishwa Bungeni

UTANGULIZI

1.          Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja kwamba Bunge lako Tukufu lipokee na kujadili Taarifa ya Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2019 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Mwaka 2020/21. Pamoja na hotuba hii ninawasilisha vitabu vya Taarifa ya Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2019 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Mwaka 2020/21. Taarifa hizi ndiyo msingi wa bajeti ya Serikali kwa mwaka 2020/21 nitakayowasilisha hapa Bungeni leo jioni.  

2.          Mheshimiwa Spika, awali ya yote nichukue fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuendelea kutujalia afya njema. Aidha, naendelea kumshukuru kwa kulijalia Taifa letu amani, utulivu na mshikamano na kutuwezesha kukutana Katika mkutano huu wa 19 na wa mwisho wa Bunge la 11 la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ili kujadili namna ya kuharakisha maendeleo ya Taifa letu.

3.          Mheshimiwa Spika, naomba nimpongeze kwa dhati Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa jinsi anavyoendelea kuliongoza vema Taifa letu. Kwa kipindi hiki cha miaka minne na nusu ya utawala wake tumeshuhudia kuimarika kwa uchumi, mfumuko wa bei umedhibitiwa, miradi mikubwa ya maendeleo inatekelezwa, uwajibikaji katika utumishi wa umma umeimarika na kero za wananchi wanyonge zinatatuliwa. Kipekee napenda kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa kuniamini kuongoza Wizara ya Fedha na Mipango tangu mwanzo wa uongozi wake hadi sasa.

4.          Mheshimiwa Spika, vile vile, napenda kuwapongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa (Mb), Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambao kwa uongozi wao mahiri wameendelea kumshauri vema Mheshimiwa Rais katika kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi mkubwa.

5.          Mheshimiwa Spika,Napenda pia kuwapongeza Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb), kwa kuteuliwa na Mheshimiwa Rais kuwa Waziri wa Katiba na Sheria pamoja na Mheshimiwa Dkt. Godwin Aloyce Mollel (Mb), kwa kuteuliwa na Mheshimiwa Rais kuwa Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto.

6.          Mheshimiwa Spika, napenda pia nitumie nafasi hii kutoa salamu za pole kwako, Waheshimiwa Wabunge na Wananchi wote kwa ujumla kwa kuondokewa na Mheshimiwa Rashid Ajali Akbar, aliyekuwa Mbunge wa Jimbo la Newala Vijijini (CCM), Mheshimiwa Mchungaji  Dkt. Getrude Pangalile Rwakatare, aliyekuwa Mbunge wa Viti Maalum (CCM), Mheshimiwa Richard Mganga Ndassa, aliyekuwa Mbunge wa Jimbo la Sumve (CCM), na Mheshimiwa Balozi Dkt. Augustine Philip Mahiga, Mbunge wa kuteuliwa (CCM) aliyekuwa Waziri wa Katiba na Sheria. Mwenyezi Mungu azilaze roho za marehemu mahali pema peponi. Amina!

7.          Mheshimiwa Spika, nchi yetu imepata mvua nyingi zilizo juu ya wastani hali iliyopelekea kutokea kwa mafuriko katika maeneo mbalimbali. Mafuriko haya yamesababisha uharibifu mkubwa wa mazao ya wakulima, mali na miundombinu hususan barabara, reli na madaraja. Mafuriko hayo yameathiri utelekelezaji wa miradi ya maendeleo na kuongeza gharama za ukarabati wa miundombinu iliyoharibika. Kwa msingi huo, katika mwaka 2020/21 kipaumbele ni kukarabati miundombinu iliyoharibika.

8.          Mheshimiwa Spika, kama unavyofahamu, nchi yetu na dunia kwa ujumla ilikabiliwa na mlipuko wa ugonjwa wa homa kali ya mapafu unaojulikana kama COVID - 19 inayosababishwa na virusi vya Corona. Ni dhahiri kuwa ugonjwa huu umeathiri uchumi wa nchi nyingi duniani kutokana na vifo, kuongezeka kwa gharama za utoaji huduma katika sekta ya afya na kuathiri shughuli za biashara na uzalishaji hususan kwa nchi zinazotegemea utalii.

9.          Mheshimiwa Spika, jambo jema ni kuwa nchi yetu haikuathirika sana na ugonjwa huu kutokana na hatua madhubuti zilizochukuliwa na Serikali ya Awamu ya Tano chini ya uongozi imara wa Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kama Taifa tuliendelea kumtegemea Mwenyezi Mungu, kuchukua tahadhari za kiafya kama inavyoshauriwa na wataalam pamoja na kufanya kazi kwa bidii. Aidha, Serikali imeendelea kuchukua hatua mbalimbali za kukabiliana na ugonjwa huu ambapo hadi sasa Serikali imetoa kiasi cha shilingi bilioni 15.49 kwa  ajili ya ununuzi wa vifaa tiba na kinga. Hatua nyingine ni pamoja na: kutolewa msamaha wa kodi kwa aina 15 za vifaa vya kupambana na COVID – 19; kutoa elimu ya jinsi ya kujikinga na maambukizi; kutenga maeneo maalum kwa ajili ya uangalizi kwa wasafiri wanaoingia nchini na wanaobainika kuwa na dalili za ugonjwa huu; na kuanzishwa kwa huduma ya namba maalum ya kupiga simu bila malipo kwa ajili ya msaada wa kiafya. Vile vile, Serikali kupitia Benki Kuu ya Tanzania imechukua hatua mbalimbali za Sera ya Fedha ili kulinda na kuimarisha uchumi zikijumuisha: kushusha kiwango cha chini cha kisheria cha sehemu ya amana kinachotakiwa kuwekwa Benki Kuu ya Tanzania kutoka asilimia 7 hadi 6; kushusha kiwango cha riba kinachotozwa kwa benki kukopa Benki Kuu kutoka asilimia 7 hadi 5; kupunguza kiwango cha dhamana za Serikali kutoka asilimia 10 hadi 5 kwa dhamana za muda mfupi na kutoka asilimia 40 hadi 20 kwa hati fungani; na kuzielekeza kampuni zinazotoa huduma za fedha kwa njia ya mtandao kuongeza kiwango cha miamala kwa siku kwa mteja kutoka shilingi milioni 3 hadi 5 na kiwango cha akiba kwa siku kwa wateja kutoka shilingi milioni 5 hadi 10.

10.      Mheshimiwa Spika, kutokana na hatua madhubuti zilizochukuliwa na Serikali, hivi sasa hali imeimarika ambapo shughuli za kiuchumi na kijamii zinaendelea kufanyika kama awali. Serikali imeruhusu vyuo vikuu vimefunguliwa, wanafunzi wa kidato cha sita wamerudi shuleni kujiandaa na mitihani, shughuli za michezo yote zimeruhusiwa,  anga limefunguliwa ambapo ndege za mizigo na abiria zinaendelea kuingia nchini na hivyo kupokelewa kwa watalii kutoka nchi mbalimbali. Hii ni ishara dhahiri ya uongozi imara wa Mheshimiwa Rais kwa Taifa hususan katika kipindi cha majanga na misukosuko mikubwa kwa dunia kama ugonjwa huu.

11.      Mheshimiwa Spika, Taarifa ya Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2019 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Mwaka 2020/21 zimezingatia dhana ya ushirikishwaji mpana wa wadau katika hatua za uandaaji na maamuzi katika ngazi zote Serikalini. Nitambue mchango mkubwa wa Bunge lako Tukufu chini ya uongozi wako Mheshimiwa Job Yustino Ndugai, Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na Mheshimiwa Dkt. Tulia Ackson, Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Aidha, napenda kumshukuru Mheshimiwa Mashimba Mashauri Ndaki (Mb), Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti na wajumbe wote wa Kamati hiyo kwa ushauri makini waliotupatia. Ushauri wao umezingatiwa kikamilifu katika uandaaji wa taarifa nilizowasilisha mbele ya Bunge hili.

12.      Mheshimiwa Spika, maandalizi ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Mwaka 2020/21 yamezingatia vipaumbele vya Serikali ya Awamu ya Tano vilivyoainishwa katika Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2016/17 – 2020/21, Ilani ya CCM ya Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2015 na ahadi za Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alizotoa wakati akifungua rasmi Bunge la Kumi na Moja. Aidha, katika mwaka 2020/21 msukumo mkubwa utawekwa katika kukamilisha utekelezaji wa miradi inayoendelea ili kupata matokeo tarajiwa.

MWENENDO WA HALI YA UCHUMI 2019

Uchumi wa Dunia

13.      Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa taarifa ya Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) ya Aprili 2020, uchumiwa dunia ulikua kwa asilimia 2.9 mwaka 2019. Aidha, uchumi wa dunia unakadiriwa kuporomoka na kufikia ukuaji wa asilimia hasi 3.0 mwaka 2020 ambao kwa kiasi kikubwa utachangiwa na athari za mlipuko wa ugonjwa wa COVID - 19. Katika mwaka 2021 uchumi wa dunia unatarajiwa kuimarika na kufikia ukuaji wa asilimia 5.8 kutokana na matarajio ya kutoweka kwa virusi vya Corona katika nusu ya pili ya mwaka 2020 na hatimaye, kuimarika kwa shughuli za kiuchumi duniani ikijumuisha biashara na uzalishaji viwandani na utekelezaji wa sera za kuongeza ukwasi katika nchi mbalimbali.

Uchumi wa Afrika na Kikanda

14.      Mheshimiwa Spika, kwa upande wa nchi za Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara, kasi ya ukuaji wa uchumi ilifikia asilimia 3.1 mwaka 2019. Matarajio ya ukuaji wa uchumi ni kupungua na kufikia wastani wa asilimia hasi 1.6 mwaka 2020 kutokana na athari za mlipuko wa ugonjwa wa COVID – 19. Aidha, ukuaji wa uchumi katika nchi za ukanda huo, unatarajiwa kuimarika na kufikia wastani wa asilimia 4.1 mwaka 2021. Ongezeko hilo litatokana na jitihada za kupambana na ugonjwa wa COVID – 19, matarajio ya kuongezeka kwa misaada kutoka nchi zilizoendelea kwa ajili ya kupambana na ugonjwa huo na matarajio ya utulivu wa bei ya nishati ya mafuta katika soko la Dunia.

15.      Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2019, uchumi wa nchi za ukanda wa Jumuiya ya Afrika Mashariki uliendelea kuimarika ambapo Tanzania ilikuwa na ukuaji wa asilimia 7.0, Rwanda asilimia 9.4, Uganda (asilimia 4.9) na Kenya asilimia 5.4. Aidha, kutokana na athari za COVID-19, ukuaji wa uchumi wa ukanda wa nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki unatarajiwa kupungua kidogo kwa mwaka 2020 na hatimaye kuanza kuimarika mwaka 2021 kutokana na juhudi zinazochukuliwa na nchi wanachama katika kupambana na athari za COVID-19 zikiwemo hatua za kifedha na kibajeti pamoja na utekelezaji wa miradi mikubwa ya maendeleo katika sekta za uchukuzi (reli, barabara na madaraja) maji, nishati, elimu na afya.

Uchumi wa Taifa

Pato la Taifa

16.      Mheshimiwa Spika, mwaka 2019, Pato la Taifa lilikua kwa asilimia 7.0 kama ilivyokuwa mwaka 2018. Ukuaji huu ulitokana na uwekezaji hususan katika miundombinu ikiwemo: ujenzi wa barabara, reli na viwanja vya ndege; kutengamaa kwa upatikanaji wa nishati ya umeme; kuimarika kwa huduma za usafirishaji; kuongezeka kwa uzalishaji wa madini hususan dhahabu na makaa ya mawe; na kuongezeka kwa uzalishaji wa mazao ya kilimo. Sekta zilizokua kwa viwango vikubwa katika kipindi hicho ni pamoja na uchimbaji madini na mawe (asilimia 17.7), ujenzi (asilimia 14.8), sanaa na burudani (asilimia 11.2), na usafirishaji na uhifadhi mizigo (asilimia 8.7). Kwa mwaka 2020, ukuaji wa Pato la Taifa unatarajiwa kupungua kidogo kutoka maoteo ya awali ya asilimia 6.9 hadi 5.5 kutokana na hatua madhubuti zilizochukuliwa na Serikali ya Awamu ya Tano chini ya uongozi wa Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania hususan kuhimiza wananchi waendelee kufanya kazi wakati wanachukua tahadhari dhidi ya corona kama inavyoelekezwa na wataalam wa afya pamoja na matarajio ya kuimarika kwa uchumi wa kikanda na dunia.

17.      Mheshimiwa Spika, mwaka 2019, Pato la wastani la kila mtu lilikuwa shilingi 2,577,967 ikilinganishwa na shilingi 2,452,406 mwaka 2018, sawa na ongezeko la asilimia 5.1. Vile vile, Pato la wastani kwa kila mtu katika dola za Marekani liliongezeka hadi kufikia dola za Marekani 1,121 mwaka 2019 kutoka dola za Marekani 1,078 mwaka 2018.

Mwenendo wa Bei

18.      Mheshimiwa Spika, mwaka 2019, mwenendo wa mfumuko wa bei uliendelea kubaki katika wigo wa tarakimu moja ambapo ulifikia wastani wa asilimia 3.4 ikilinganishwa na wastani wa asilimia 3.5 mwaka 2018. Mfumuko wa bei za nishati umeendelea kupungua na kufikia asilimia 4.1 Aprili 2020 kutoka asilimia 13.3 Aprili 2019 kutokana na kupungua kwa bei za nishati ya mafuta katika soko la dunia.

Utekelezaji wa Sera ya Fedha 2019/20

19.      Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Benki Kuu imeendelea kutekeleza sera ya fedha ya kuongeza ukwasi kwenye uchumi ambayo imesaidia kupunguza viwango vya riba katika masoko ya fedha hususan riba za mikopo na amana. Wastani wa riba za mikopo ya benki kwa ujumla katika kipindi cha Julai 2019 hadi Aprili 2020 ulipungua hadi asilimia 16.85 ikilinganishwa na wastani wa asilimia 17.16 katika kipindi kama hicho mwaka 2018/19, na riba za mikopo ya kipindi cha mwaka mmoja zimepungua na kufikia wastani wa asilimia 16.24 kutoka asilimia 17.79. Vile vile, wastani wa riba za amana kwa ujumla ulikuwa asilimia 7.02 katika kipindi cha Julai 2019 hadi Aprili 2020, ikilinganishwa na wastani wa asilimia 7.62 katika kipindi kama hicho mwaka 2018/19. Aidha, riba za amana za kipindi cha mwaka mmoja ziliongezeka na kufikia wastani wa asilimia 8.77 katika kipindi cha Julai 2019 hadi Aprili 2020 kutoka wastani wa asilimia 8.21 katika kipindi kama hicho mwaka 2018/19.

Ujazi wa Fedha na Karadha

20.      Mheshimiwa Spika, Katika kipindi cha Julai 2019 hadi Aprili 2020, wastani wa ukuaji wa ujazi wa fedha kwa tafsiri pana zaidi (M3) uliongezeka kwa asilimia 9.9 na kufikia shilingi trilioni 28.8 mwezi Aprili 2020 kutoka shilingi trilioni 25.6 mwezi Aprili 2019. Ongezeko hili la ujazi wa fedha ni matokeo ya utekelezaji thabiti wa sera ya fedha, ongezeko la mikopo kwa sekta binafsi pamoja na rasilimali fedha za kigeni katika sekta ya benki.

Mwenendo wa Mikopo kwa Sekta Binafsi

21.      Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha Julai 2019 hadi Aprili 2020, wastani wa ukuaji wa mikopo kwa sekta binafsi ulikuwa asilimia 8.7 kufikia shilingi trilioni 19.7 ikilinganishwa na shilingi trilioni 18.6 Aprili 2019. Sehemu kubwa ya mikopo ilielekezwa kwenye shughuli binafsi (asilimia 31.1) ikifuatiwa na shughuli za biashara asilimia 17.6, uzalishaji viwandani asilimia 11.0 na kilimo asilimia 7.7.

Sekta ya Nje

22.      Mheshimiwa Spika, hadi Aprili 2020, urari wa jumla wa malipo ulikuwa na ziada ya dola za Marekani milioni 897.1 ikilinganishwa na nakisi ya dola za Marekani bilioni 1.1 katika kipindi kama hicho mwaka 2019. Hii ilichangiwa na kupungua kwa nakisi ya urari wa biashara ya bidhaa, huduma na uhamisho wa mali nchi za nje kulikotokana na kuongezeka kwa mauzo ya bidhaa nje ya nchi.

23.      Mheshimiwa Spika, nakisi kwenye urari wa biashara ya bidhaa, huduma na uhamisho mali nchi za nje ulipungua hadi kufikia dola za Marekani milioni 333.3 mwezi Aprili 2020, ikilinganishwa na nakisi ya dola za Marekani bilioni 1.6 katika kipindi kama hicho mwaka 2019. Kupungua huku kulitokana na kuongezeka kwa mauzo ya bidhaa nje ya nchi, hususa katika bidhaa asilia na zisizo asilia kama vile dhahabu.

24.      Mheshimiwa Spika, hadi Aprili 2020, mauzo ya bidhaa na huduma nje yaliongezeka kufikia dola za Marekani bilioni 8.6 ikilinganishwa na dola za Marekani bilioni 7.3 Aprili 2019. Hii ilichangiwa na kuanzishwa kwa masoko ya madini nchini kulikopelekea kuongezeka kwa mauzo ya dhahabu sanjari na ongezeko la bei katika soko la dunia. Thamani ya uagizaji bidhaa na huduma kutoka nje ya nchi ilikuwa dola za Marekani bilioni 8.6, ikilinganishwa na dola za Marekani bilioni 8.7 katika kipindi kama hicho mwaka 2019. Sehemu kubwa ilitumika katika uagizaji mafuta na bidhaa za mitaji ikiwemo mitambo na mashine inayotumika katika utekelezaji wa miradi mikubwa ya miundombinu ya reli, barabara, madaraja na uzalishaji umeme.

Akiba ya Fedha za Kigeni

25.      Mheshimiwa Spika, hadi Aprili 2020, akiba ya fedha za kigeni ilifikia dola za Marekani bilioni 5.3, kiasi kinachotosheleza kulipia uagizaji wa bidhaa na huduma kutoka nje ya nchi kwa kipindi cha miezi 6.1. Kiwango hiki ni zaidi ya lengo la nchi la miezi 4.0, ambayo ni juu ya lengo la nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki la miezi isiyopungua 4.5 na Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika la miezi isiyopungua 6.0.

Mwenendo wa Thamani ya Shilingi

26.      Mheshimiwa Spika, thamani ya shilingi ya Tanzania dhidi ya sarafu nyingine kubwa duniani imeendelea kuwa tulivu kwa kipindi chote cha mwaka 2019/20. Katika kipindi cha Julai 2019 hadi Aprili 2020, dola moja ya Marekani ilibadilishwa kwa wastani wa kati ya shilingi 2,299.3 na shilingi 2,302.7 katika soko la fedha la jumla ikilinganishwa na wastani wa kati ya shilingi 2,276.4 na shilingi 2,300.9 kwa dola moja ya Marekani katika kipindi kama hicho mwaka 2018/19.

Deni la Serikali

27.      Mheshimiwa Spika, hadi Aprili 2020, deni la Serikali lilifikia shilingi trilioni 55.43. Kati ya kiasi hicho, deni la nje lilikuwa shilingi trilioni 40.57 na deni la ndani shilingi trilioni 14.85. Deni la Serikali lilichangiwa na kupokelewa kwa mikopo mipya kwa ajili ya kugharamia miradi mbalimbali ya maendeleo inayochochea kasi ya ukuaji wa uchumi. Matokeo ya tathmini ya uhimilivu wa deni iliyofanyika Desemba 2019, imeonesha kuwa deni la Serikali ni himilivu katika kipindi cha muda mfupi, wa kati na mrefu.

Utafiti wa Sekta Isiyo Rasmi    

28.      MheshimiwaSpika, mwaka 2019/20, Serikali ilifanya utafiti wa Sekta Isiyo Rasmi mkoani Dar es Salaam kwa lengo la kubaini mchango wa sekta hiyo kwenye Pato la Taifa kwa kutumia makadirio ya mapato na ongezeko la thamani ya uzalishaji wa bidhaa na huduma kutoka shughuli za kilimo na zisizo za kilimo; tija katika uwekezaji; kiwango cha ukuzaji mtaji; kutambua mahali biashara zilipo; thamani ya uzalishaji kwa kila mtu; ajira na mgawanyo wake; na mahusiano kati ya Sekta Isiyo Rasmi na sekta nyingine za kiuchumi.

29.      MheshimiwaSpika, matokeo ya utafiti huo yanaonesha kuwa: Mkoa wa Dar es Salaam una wamiliki wa shughuli za Sekta Isiyo Rasmi wapatao 1,023,520 ambapo asilimia 47.6 wanajihusisha na biashara ya jumla na rejareja pamoja na matengenezo ya magari na pikipiki;   uwekezaji wa mitaji katika sekta isiyo rasmi ni shilingi bilioni 901.5 kwa mwaka 2019; jumla ya ongezeko la thamani kwa mwaka katika bidhaa na huduma zinazozalishwa katika sekta isiyo rasmi ni shilingi trilioni 6.2; na ajira katika sekta isiyo rasmi kwa watu wenye umri wa miaka 15 au zaidi imepungua kutoka watu 1,208,250 (asilimia 61.5) mwaka 2014 hadi 1,154,336 (asilimia 55.2) mwaka 2019. Hii inatokana na juhudi kubwa za Serikali ya Awamu ya Tano katika kupanua wigo wa kujenga uchumi wa viwanda ambao matokeo yake ni kukuza upatikanaji wa kazi zenye staha (decent work) na kuongezeka kwa ajira katika sekta rasmi.

30.      Mheshimiwa Spika, maelezo ya kina kuhusu hali ya uchumi yapo katika Aya ya 9 hadi 26 ya hotuba yangu na kitabu cha Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2019.

MAFANIKIO YA UTEKELEZAJI WA MPANGO KWA KIPINDI CHA 2016/17 – 2019/20

31.      Mheshimiwa Spika,


This post first appeared on MASWAYETU, please read the originial post: here

Share the post

Taarifa Ya Hali Ya Uchumi Wa Taifa Kwa Mwaka 2019 Na Mpango Wa Maendeleo Wa Taifa Wa Mwaka 2020/21 Wawasilishwa Bungeni

×

Subscribe to Maswayetu

Get updates delivered right to your inbox!

Thank you for your subscription

×