Get Even More Visitors To Your Blog, Upgrade To A Business Listing >>

Tume Ya Kurekebisha Sheria Yakabidhi Ripoti Ya Mapendekezo Sheria Ya Ufilisi

Tags: sheria ufilisi
Waziri wa Katiba na Sheria Dkt Balozi Augustine Mahiga amepokea ripoti ya mapendekezo ya sheria yaliyowasilishwa na Tume ya Kurekebisha Sheria hii leo Jijini Dodoma.

Akipokea taarifa hiyo Dkt Balozi Mahiga amefurahishwa kwa kazi nzuri iliyofanywa na Tume hiyo pamoja na wadau mbalimbali waliofanikisha kukamilika kwa mapendekezo ya sheria ya Ufilisi na nyingine zilizowasilishwa katika tume hiyo  ambazo ni sheria ya Ushahidi na ile ya Mamlaka ya Hifadhi ya  Ngorongoro.

‘’Nimeridhishwa kwa kazi nzuri iliyofanyika kwani tunakwenda kupata sheria madhubuti itakayoendana na hali ya sasa na kusimamia kikamilifu misingi ya utawala bora’’. Alisema Balozi Mahiga.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Tume ya Kurekebisha Sheria Mhe, Januari  Msofe amesema kuwa tume yake imefanya mapitio na utafiti wa kina kuhusu mifumo ya  Sheria zinazosimamia Ufilisi na kubaini mapungufu ya kisheria na kiutendaji ambao umeathili utekelezaji wa masuala ya hayo hapa Nchini.

Ameendelea kubainisha mapungufu hayo ni pamoja na kuwepo kwa sheria mbalimbali za kisekta kama vile sheria ya Makampuni sura ya 212, sheria ya mabenki na taasisi za kifedha sura ya 342 , sheria ya vyama vya ushirika sura ya 211, Sheria ya bima sura ya 394, sheria ya mashirika ya umma Sura ya 57  na sheria ya usajili wa wadhamini sura ya 318 na hivyo kukosekana kwa sheria mahsusi inayosimamia jukumu la ufilisi pekee na kusababisha mkanganyiko kwa watumiaji kufanya maamuzi ya sheria ipi inaweza kutatua matatizo yanayowakabili.

Hata hivyo kuwepo kwa sheria hizo kumesababisha matatizo kwa wadai kutojua taratibu za kupata haki zao kwa wakati pamoja na kuwepo kwa taratibu ndefu zinazochelewesha mashauri ya ufilisi kumalizika kwa wakati mara baada ya taasisi au kampuni husika kufilisika.

Ameongeza kuwa Sheria zinazotumika hivi sasa zimepitwa  na wakati ambazo baadhi yake zinatoa adhabu na faini ndogo kwa wale wanaokiuka taratibu za ufilisi kwa mfano faini ya shilingi 200 kiasi ambacho hakiendani na kiwango cha uchumi na maisha ya sasa huku zikitambua njia moja tu ya mawasiliano ambayo ni  posta pekee huku ikiacha nyuma maendeleo makubwa upande wa teknolojia ya habari na mawasiliano.

Vilevile Ugumu wa taratibu za kisheria katika ufilisi wa makampuni ya nje yenye kampuni tanzu Tanzania na hivyo kuziachia kampuni hizo kutumia sheria za nchi zao na kusababisha tatizo la kiuchumi katika nchi yetu kutokana na sheria zetu kukosa nguvu ya kuyadhibiti makampuni hayo tofauti na nchi jirani ya Kenya na Uganda ambazo zimeweka sheria na taratibu nzuri za kufuata kwa makampuni ya nje yenye kampuni tanzu kwenye nchi zao.

Mapungufu ya sheria hizo pia kumesababisha Kuwepo kwa mamlaka na vyombo mbalimbali vinavyosimamia masuala ya ufilisi kama vile kuangalia mali za kampuni pale inapofikia hatua ya kufilisika na mahakama kuteua chombo au taasisi yoyote inayoshughulika na ufilisi badala ya Taasisi ya RITA ambayo kisheria ndiyo yenye mamlaka kisheria ya kuwa msimamizi na mratibu wa masuala yote ya ufilisi.

Hafla ya kukabidhi ripoti hiyo ilihudhuriwa na baadhi ya Wakuu wa Taasisi, Watumishi wa Wizara ya katiba na sheria, Wakala wa Usajili Ufilisi na Udhamini, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu pamoja Wizara ya Ardhi.




This post first appeared on MASWAYETU, please read the originial post: here

Share the post

Tume Ya Kurekebisha Sheria Yakabidhi Ripoti Ya Mapendekezo Sheria Ya Ufilisi

×

Subscribe to Maswayetu

Get updates delivered right to your inbox!

Thank you for your subscription

×