Get Even More Visitors To Your Blog, Upgrade To A Business Listing >>

DC acharuka mimba ya mwanafunzi



MKUU wa wilaya ya Bunda mkoani Mara, Lydia Bupilipili ameliagiza jeshi la polisi wilayani humo, kumkamata mwenyekiti wa kijiji cha Karukekerere, Nyandago Magesa, kwa tuhuma za kuzuia mwanaume aliyempa ujauzito mwanafunzi wa kidato cha pili katika shule ya sekondari Muranda asikamatwe.

Mkuu Huyo wa wilaya alitoa agizo hilo jana kwenye kikao cha wadau wa maendeleo wa wilaya ya Bunda, kilichofanyika katika ukumbi wa halmashauri mjini hapa. Bupilipili alitoa agizo hilo baada ya Diwani wa Kata ya Namhura Jogoro Amoni kuibua hoja hiyo katika kikao hicho.

Diwani huyo alisema Kuwa katika kata yake kuna mwanaume mmoja anayetambulika kwa jina la Zephania Masolo, amempatia ujauzito mwanafunzi wa kidato cha pili, anayesoma katika shule ya sekondari Muranda, iliyoko katika kata ya Namhura wilayani Bunda.

Amoni alisema kuwa pamoja na taarifa hiyo kuripotiwa katika ofisi ya serikali ya kijiji hicho na ofisi ya kata hiyo, mgambo walipokwenda kumkamata mtuhumiwa, mwenyekiti huyo aliwazuia kufanya hivyo kwa kile kinachodaiwa kuwa ni rafiki yake.

Alisema kuwa alishangazwa na kitendo mwenyekiti huyo kuwazuia mgambo kumkamata Mtuhumiwa Huyo, huku akijua fika kuwa kosa alilofanya ni kubwa na yeye ni kiongozi wa serikali ya kijiji anapaswa kukemea vitendo hivyo ndani ya jamii ili visitokee tena.

Amoni alisema kuwa kiongozi huyo alitakiwa kuonyesha mfano wa hali ya juu katika kulitatua suala hilo ili liweze kuwa fundisho kwa wanaume wengine wanaotumia mwanya kurubuni watoto wa kike na kuwapa ujauzito.
Aidha alikiambia kikao hicho kuwa yuko tayari kutoa ushirikiao wa kutosha kwa mkuu wa wilaya hiyo ili mtuhumiwa huyo aweze kukamatwa.
Aliongeza kuwa yuko tayari kutoa ushirikiano wa kutosha ili mtuhumiwa huyo aweze kukamatwa maana kitendo hicho kimekera wananchi wengi wa kata yake wakiwemo walimu, wanafunzi na wazazi.
Baada ya taarifa hiyo kutolewa mkuu wa wilaya alieleza kukerwa na kitendo hicho na akamuagiza mkuu wa polisi wilayani hapa, kuhakikisha mtuhumiwa huyo anakamatwa mara moja pamoja na mwenyekiti wa kijiji hicho.
“OCD uko hapa na wewe ni mjumbe wa kamati ya ulinzi na usalama nina kuagiza mtuhumiwa huyo akamatwe mara moja pamoja na huyo mwenyekiti aliyewazuia mgambo kumkamata,” alisema Bupilipili na kuongeza kuwa suala hilo haliwezi kufumbiwa macho na serikali, kwani ni kitendo ambacho kinaikera serikali kuona wanafunzi wanakatishwa masomo na kuharibu ndoto za maisha yao ya baadaye.

Alisisitiza kuwa ni lazima wazazi, walezi na wananchi kwa ujumla, kuwekeza kwenye elimu na kwamba suala la elimu halina mzaa kabisa katika wilaya hiyo na taifa kwa ujumla.

Bupilipili alisema kuwa wanaume wanaojidanganya kwamba serikali imelala na kuendelea kuwachezea wanafunzi na kuwapa ujauzito wasome nyakati za majira, kwani siku zao zinahesabika na watatiwa mbaroni wakati wowote kuanzia sasa.


This post first appeared on MASWAYETU, please read the originial post: here

Share the post

DC acharuka mimba ya mwanafunzi

×

Subscribe to Maswayetu

Get updates delivered right to your inbox!

Thank you for your subscription

×