Get Even More Visitors To Your Blog, Upgrade To A Business Listing >>

KWANINI WANAUME WANAPATA TATIZO LA HAJA NDOGO?


Mungu alimwumba mtu  kwa mfano wake.  Wakati wa uumbaji mtu alikuwa mkamilifu machoni pa Muumbaji  na Ulimwengu.  “nitakushukuru kwa sababu nimeumbwa kwa jinsi ya ajabu na ya kutisha” hivyo ndivyo mfalme Daudi alivyoelezea kicho chake kwa Mungu aliyemwumba mwanadamu (Zaburi 139:14).  Dhambi iliingia na kwa kuingia kwa dhambi yakaja na mateso ya aina mbalimbali.

Kujaribu kujibu swali hilo hapo juu bila kuonesha anatomi ya Mfumo wa Mkojo wa Mwanamme kutamuacha msomaji na maswali yasiyojibiwa na taarifa zisizo wazi.  Hivyo hebu tujifunze anatomi ya mfumo wa mkojo kama ulivyoumbwa na Mungu.


Moyo husukuma damu kwenda katika viungo vyote vya mwili.  Damu inabeba hewa ya oksijeni na chakula kwa seli za mwili.  Hewa ya oksijeni inatumika kama nishati ya kuunguza chakula ambacho nacho huzalisha nishati ili kutegemeza seli za mwili.  Kama gari linavyounguza mafuta ili kupata nishati ya kuliendesha, seli pia huunguza chakula kwa kutumia hewa ya oskijeni ili kupata nishati muhimu kwa matumizi yake.

Wakati wa hatua hiyo ya kuunguza chakula, uchafu (ambao kama ukiachwa kulundikana mwilini ungeweza kuwa sumu kwa seli) huwa unazalishwa.

Mungu katika hekima yake aliumba figo ili kuchuja takataka (sumu) kutoka na kuziondoa mwilini.  Damu inaingia kwenye figo kupitia mishipa ya ateri za mafigo.  Damu inachujwa na kuondolewa sumu zote.  Maji yaliyochujwa yanayeyusha takataka zilizochujwa na kuzalisha mkojo.  Mkojo husafirishwa kupitia ureta mpaka kwenye Kibofu ili kuhifadhiwa.  Wakati kibofu kinakuwa kimejaa (ujazo ni karibu mililita 500), hisia hufanyizwa ambayo husababisha haja ya kutaka kukojoa.  Ndipo mtu anakwenda mahali panapokubalika kijamii, na anapokuwa tayari misuli ya kibofu hukaza, na musulibanifu (kilango) hufunguka na shinikizo linalosababishwa na kukaza kwa kibofu hulazimisha mkojo kutoka kupitia katika urethra (ujia wa kutolea mkojo).  Wakati kibofu kinapokuwa tupu musulibanifu hufunga na adha ya kibofu kilichojaa inapungua.

Wanaume wengi wanapata mabadiliko ya mkojo kadri wanavyokuwa wazee, mabadiliko yanayoweza kusababishwa na uvimbeuchungu au ukuaji wa tezi ya prosteti (BPH) ni moja tu ya sababu za dalili za matatizo katika mfumo wa mkojo.  Hivyo hebu nianze kueleza kwa ufupi tezi ya prosteti ni nini.  Chini ya Kibofu Cha Mkojo kuna tezi ya prosteti ambayo inapatikana tu kwa wanaume.  Kabla ya baleghe tezi hii huwa ni ndogo sana lakini baada ya hapo inaanza kukua kwa kasi kutokana na mchocheo wa homoni ya kiume iitwayo “testosterone”.  Ujia wa urethra unapitia katika tezi ya prosteti.  Kadiri ya mtu anavyo ongezeka umri tezi ya prosteti inakuwa kubwa zaidi na zaidi.  Inaweza kuongezeka ukubwa bila kuwa na ugonjwa ndani yake au inaweza ikakua ikiwa na ugonjwa ndani yake (mfano saratani).  Kadiri inavyokuwa kubwa zaidi inaufanya ujia wa urethra kuwa mwembamba.  Kubanwa kwa ujia wa kupitia mkojo husababisha matatizo katika kutoa haja ndogo.

Matatizo haya yanaweza kuanza mapema katika umri wa miaka arobaini (40) na kwa nadra sana hutokea kabla ya miaka arobaini.  Waathiriwa wengi wa tatizo hili katika mazingira yetu ya Afrika ni kati ya umri wa miaka 55 mpaka 70.

Je, Ni Matatizo Gani Ambayo Hawa Wanaume Wenye Tezi Kubwa ya Prosteti Hukabiliwa Nayo?

Sio dalili zote za haja ndogo zinatokana na mabadiliko katika tezi ya prosteti.  Aidha kuna wanaume wenye tezi kubwa ya prosteti na bado wanapata dalili chache tu za matatizo ya mkojo kama zipo.

Dalili za matatizo ya mfumo wa mkojo zinazojitokeza kwa kawaida ni:
a.       Mchirizi dhaifu na unaokatizwa wa mkojo.
b.      Tatizo la kuanza kukojoa hata wakati kibofu kimejaa.
c.       Hisia kuwa kibofu bado hakijatoa mkojo wote.
d.      Hitaji la kukojoa mara kwa mara wakati wa mchana na wakati wa usiku.
e.      Hitaji la kukojoa mara moja au papo kwa papo mara tu unapohisi kubanwa.
f.        Kuendelea kudondoka kwa mkojo baada ya kukojoa.
g.       Kujisikia kuunguzwa au maumivu wakati wa kukojoa.

Wanaume wengine wanakuja hospitalini wakiwa na maumivu makali ya kuzuiliwa mkojo ndani ya kibofu.  Hali hii ni ya maumivu sana na inahitaji huduma ya haraka ya kiafya ili kuepuka uharibifu wa figo, nk.  Wanaume wengine wanakuja wakiwa na matatizo ya uzuiaji sugu wa mkojo.  Taratibu huwawia vigumu zaidi kukojoa mkojo wote, na mkojo mwingi zaidi hubakia kwenye kibofu baada ya kwenda msalani.  Athari zingine za tatizo hili ni pamoja na: uambukizo wa mara kwa mara wa kibofu cha mkojo, na kufanyizwa vijiwe ndani ya kibofu cha mkojo.

Ni muhimu kumwambia daktari wako matatizo ya mkojo kama yalivyoelekezwa hapo juu.  Katika wagonjwa 8 kati ya 10, dalili hizi huashiria dalili za BPH, lakini pia zinaweza kuashiria matatizo mengine makubwa zaidi yanayohitaji matibabu ya haraka.  Hali hizi, ikiwa ni pamoja na saratani ya tezi ya prosteti, zinaweza tu kufutiliwa mbali kwa uchunguzi wa daktari.


This post first appeared on Afya Na Kiasi, please read the originial post: here

Share the post

KWANINI WANAUME WANAPATA TATIZO LA HAJA NDOGO?

×

Subscribe to Afya Na Kiasi

Get updates delivered right to your inbox!

Thank you for your subscription

×