Get Even More Visitors To Your Blog, Upgrade To A Business Listing >>

USUGU WA BAKTERIA, JANGA LINALOHITAJI ELIMU YA AFYA KUKABILIANA NALO




Matumizi ya Dawa za antibiotiki yasiyozingatia maelekezo ya daktari hufanya vimelea kuwa sugu, Shirika la Afya Duniani (WHO) limesema.  Tahadhali hii inatolewa baada ya shirika hilo kuorodhesha bakteria sugu wasiotibika kwa dawa zilizopo.
Kutokana na kushamiri kwa matumizi ya dawa hizi, baadhi ya wagonjwa wamekuwa wakizitumia bila kufuata utaratibu unaoshauriwa hivyo hivyo kuongeza usugu wa vimelea ambao ni tatizo jingine kwa afya ya binadamu.
WHO inatahadharisha, iwapo hatua stahiki hazitachukuliwa, hadi kufikia mwaka 2050, tatizo hilo linaweza kusababisha vifo vya zaidi ya watu milioni 10 kila mwaka.
Shirika hilo linatoa wito, kila mtu kuchukua hatua ikiwamo kuepuka matumizi ya dawa za antibiotiki kama hakuna ulazima wa kufanya hivyo, kwa sababu si kila ugonjwa anazitegemea kwa tiba, mfano mafua.
Namna sahihi ya kutumia Dawa Hizo, WHO inaelekeza, ni lazima iwe kwa kufuata maelekezo ya daktari.  “haishauriwi kukatisha kutumia dawa kabla ya kupona kabisa,” linasema shirika hilo.
Miongoni mwa tahadhali inayotolewa na WHO kuhusu dawa hizi ni pamoja na kutozihifadhi kwa matumizi ya watu wengine.
Wataalamu wamekwenda mbele zaidi kuhusu usugu wa dawa za antibiotiki kwamba unachangiwa na ulaji wa nyama ya mnyama aliyetibiwa kwa dawa hizo, hivyo sekta za kilimo na mifugo zinachangia kwa kiasi kikubwa usugu wa dawa hizo kwa binadamu.
Mganga mkuu wa Serikali, Profesa Muhammed Kambi Anasema Wizara ya Afya imeingia rasmi kwenye mapambano dhidi ya suala hilo.  Anasema binadamu anaathirika zaidi na usugu wa vimelea kutokana na kuzitumia kwa wingi kutoka kwenye mifugo kwa sababu hutumika kuwatibu kabla hawajachinjwa na kuliwa.
Anafafanua, binadamu akinywa maziwa ya ng’ombe aliyetibiwa kwa dawa za antibiotiki au akila nyama ya mnyama aliyetibiwa kwa dawa hizo huwa ngumu kutibika antibiotiki kwa sababu bakteria wanakuwa wameizoea dawa na kujipanga kupambana nayo.
“Kwa magonjwa yanayoambukiza kwa njia ya hewa kutoka kwa mgonjwa mmoja kwenda kwa mwingine, bakteria wa mgonjwa aliyepata usugu wa dawa vikienda kwa mtu mwingine havitatibika kwa sababu vitakuwa vimehama vikiwa sugu,” anasema Profesa Kambi.
Serikali imezindua mpango kazi wa miaka mitano kupambana na usugu wa dawa hizo unaowahusisha wataalamu kutoka idara tofauti zikiwamo kilimo, mifugo na afya kujadili namna Tanzania itakavyokabiliana na usugu huo.  Mpango huo unatekelezwa kuanzia mwaka huu hadi 2022.
Mganga mkuu huyo anasema Serikali itashiriki kwa kufanya utafiti wa dawa na chanjo, kuvutia wawekezaji kuwekeza kwenye dawa na vifaa tiba.
Mkuu wa Sekta ya Afya ya Ubalozi wa Uswisi, Thomas Teuscher anasema ipo haja kwa wadau wa sekta binafsi na umma kuungana ili kukabiliana na janga hilo kwa sababu linagusa wengi.
Anasema Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA) inatakiwa kuongeza umakini wa ukaguzi ili kuhakikisha dawa bandia haziingii nchini kwa sababu huchangia kurudisha nyuma juhudi za kupambana na usugu huo.
Anasema kutumia dawa za antibiotiki kiholela, kutomaliza dozi iliyopendekezwa na kutumia dawa bandia kunachangia usugu na huchukua muda kubainika.
Dawa feki za antibiotiki zinapotumika, anasema, zinajenga usugu wa mgonjwa anapotumia dawa halisi hawezi kupona kwa sababu hapo awali hakutumia dawa sahihi.
“Kwa sababu wao ndiyo wana jukumu la kusimamia uhakika wa dawa, wana nafasi kubwa kwenye mapambano haya ya matumizi sahihi ya dawa za antibiotiki,” anasema Teuscher.
Mwakilishi wa WHO nchini, Dk Richard Banda anazitaja familia 12 za bakteria ambazo zinahitaji dawa mpya kutokana na zilizokuwapo kutokuwa na makali yanayohitajika.
Anasema WHO imetoa orodha ya bakteria hao ili kuwapa mwanya watafiti, Serikali na wadau wa sekta ya afya kutafuta mbadala wa dawa hizo.
Baadhi ya bakteria waliomo kwenye orodha isiyotibika kuwa ni pamoja na waliokuwa wanatibiwa kwa dawa za mchafuko wa tumbo, maambukizi katika njia ya mkojo na kaswende.
“Orodha hii itahamasisha na kuwashawishi watengenezaji wa dawa kubuni aina mpya,” anasema Dk Banda.
Mkurugenzi wa Huduma za Mifugo wa Wizara ya Kilimo na Mifugo, Dk Abdu Hayghaimo anawataka wazalishaji wa vyakula vya mifugo kutumia vifaa vya asili kutengeneza dawa badala ya kemikali.
Pia anataka mamlaka husika kufanya ukaguzi wa mara kwa mara ikiwamo kuchukua sampuli za vyakula vya mifugo kama vinakidhi viwango.
Katika kuhakikisha mpango kazi huo unaeleweka vema kabla ya kuanza kuufanyia kazi, Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Wazee na Watoto, Dk Mpoki Ulisubisya anasema baadhi ya malengo ya mpango huo wa miaka mitano ni pamoja na kutoa elimu kwa jamii.
Anasema wahusika watafanya utafiti wa kuangalia namna sahihi ya kupunguza maradhi yanayosababishwa na bakteria sugu na kuelimisha kuhusu matumizi sahihi ya dawa hizo kwa binadamu na wanyama ili kupunguza mwingiliano unaosababisha usugu kutokana na wanyama na mimea.
“Mpango utaangalia jinsi ya kuongeza upatikanaji, utafiti wa dawa; za zamani na mpya, upatikanaji wa vifaa tiba, chanjo na njia nyingine mbalimbali za kukabiliana na tatizo hili,” anasema Dk Ulisubisya.
Anafafanua kuwa mpango kuelekeza maeneo ya vipaumbele na namna ya utekelezaji.  Mwaka 2000, anasema usugu wa dawa hizo ulikuwa asilimia 20 tu nchini lakini sasa ni asilimia 80.
Baada ya kuona ongezeko la tatizo hilo kwenye mataifa mengi, anasema WHO imeandaa One Health, na Wizara nayo kuja na mpango utakaosaidia kuwaunganisha wataalamu kutambua njia sahihi za kukabiliana na tatizo hilo.
“Shida tuliyonayo ni usugu ambao umeanza kuonekana kwenye dawa nyingi kwa kasi kubwa kuliko uwezo wa wataalamu kugundua dawa nyingine zinazoweza kutibu maradhi hayo,” anasema.
Baadhi ya athari zitakazojitokeza kutokana na usugu huu wa dawa ni kuongezeka kwa gharama za matibabu kunakotokana na kuugua muda mrefu au kutumia dawa ghali ili kudhibiti zilizozoeleka.
Athari nyingine ni kutumia muda mwingi kwenye matibabu hivyo kutojishughulisha na uzalishaji mali, na kuongezeka kwa hatari ya kupoteza maisha endapo dawa stahiki hazitopatikana.
Katibu mkuu huyo, anasema mpango huo utasaidia kuongeza hamasa kwa watafiti na watengenezaji wa dawa kuongeza jitihada za uvumbuzi wa dawa mpya zitakazokuwa na tija.   


This post first appeared on Afya Na Kiasi, please read the originial post: here

Share the post

USUGU WA BAKTERIA, JANGA LINALOHITAJI ELIMU YA AFYA KUKABILIANA NALO

×

Subscribe to Afya Na Kiasi

Get updates delivered right to your inbox!

Thank you for your subscription

×