Get Even More Visitors To Your Blog, Upgrade To A Business Listing >>

HARUFU MBAYA YA KINYWA HAITIBIWI KWA DAWA ZA MENO


Wapo watu wana Harufu Mbaya ya kinywa kiasi cha kukosa amani mbele ya hadhara.  Hawa ni wale wanaotambua juu ya tatizo hilo.  Wengine hawaelewi lakini huwa kero kwa jamaa zao wanaolazimika kuwa wavumilivu ili kutoharibu uhusiano uliopo.

Harufu mbaya ya kinywa inaweza kuwa tatizo linalokukera hata kukusababishia wasiwasi unapojumuika na wenzako katika masuala mbalimbali, iwe ofisini au mtaani.

Kitu ambacho wengi hawafahamu ni kwamba dawa nyingi zinazouzwa na kuelezwa kutibu tatizo hilo hazina uwezo wa kuleta suluhu ya kudumu bali ya muda mfupi tu.  Dawa hizo hazitibu tatizo bali linagusa tu athari zake.

Usishangae kwa sababu ya uwapo wa dawa kadha wa kadha zilizotengezwa kwa ajili ya kupambana na harufu ya kinywa.  Dawa hizi hazijaelekezwa kwenye kiini cha tatizo bali linapoishia.

Ili kumaliza harufu ya kinywa ni lazima kujua imesababishwa na nini ambacho kitadhibitiwa kikamilifu ili kupata suluhu ya kudumu.  Zipo sababu nyingi zinazochangia harufu hii.

Baadhi ya vyakula, magonjwa au tabia huweza kusababisha harufu mbaya ya kinywa.  Pamoja na hayo habari njema ni kwamba unaweza kuondokana na kadhia hiyo kwa kufanya usafi madhubuti wa kinywa chako.

Ili kukabiliana na tatizo hili inashauriwa kuwa macho wakati wote.  Hili litafanikiwa endapo utazifahamu dalili za kuwa na harufu isiyopendeza kutoka kinywani mwako.  Lakini ni muhimu kufahamu kwamba harufu mbaya hutofautiana kutegemea chanzo.

Kuna baadhi ya watu wana mashaka na harufu ya vinywa vyao hata kama wana tatizo wakati wapo wenye harufu mbaya ila hawajitambui.

Kwa sababu ni vigumu kutathmini harufu ya kinywa chako mwenyewe, unaweza kumuuliza mtu wako wa karibu ili kujiridhisha kama una harufu mbaya ya kinywa.

Ukithibitisha kuwa nayo, ni vyema ukapitia ufanyaji wako wa usafi wa kinywa.  Jaribu kufanya mabadiliko ya mfumo wa maisha kama vile kupiga mswaki mara baada ya kula na kunywa maji mengi.

Ukiona tatizo linaendelea licha ya kufanya mabadiliko haya, ni vyema ukamuona daktari wa kinywa na meno kwa msaada zaidi.  

Ni daktari huyu pekee anapaswa kukueleza chanzo cha tatizo hilo ambalo mara nyingi huwa linatokana na matatizo yaliyomo kinywani.

Uchunguzi wa daktari wa kinywa na meno unaweza ukakupeleka kwa madaktari wengine kwa uchunguzi zaidi kama ataona tatizo lako halitokani na hali ya afya ya kinywa chako.

Sababu

Mara nyingi harufu mbaya ya kinywa huanzia mdomoni ingawa vyanzo vyake ni vingi.  Ugonjwa wa fizi ni moja ya sababu ya harufu hii kwani husababisha kuvimba na kutoa damu wakati wa kupiga mswaki, kung’ata kitu ama kutema mate.

Ugonjwa wa fizi hutokana na upigaji wa mswaki.  Wakati mwingine huwa hauna maumivu kiasi kwamba mtu anaweza kuwa nao na asijue.

Kutopiga mswaki ni sababu nyingine.  Kama hupigi mswaki na kufanya flosi, mabaki ya chakula yakikaa kwa muda huoza na kutoa harufu mbaya.  Ulimi nao unastahili kufanyiwa usafi kwani unafanana na taulo hivyo kushika mabaki ya chakula na kuweza kukaribisha bacteria baada ya kula.

Meno ya Bandia

Meno ya bandia yasiyosafishwa mara kwa mara au ambayo hayakai vizuri huweza kuhifadhi mabaki ya chakula na bacteria ambao kwa pamoja huweza kuchangia kuwapo kwa harufu mbaya ya kinywa.

Meno Yaliyotoboka

Meno yaliyotoboka hayasafishiki unapopiga mswaki.  Matundu yaliyopo kwenye meno hayo huweza kuhifadhi chakula ambacho baada ya muda huoza na kutoa harufu mbaya.

Japokuwa tatizo hili husababishwa na meno yote yaliyotoboka, lakini ya nyuma (magego) huchangia zaidi kwani mara nyingi watu wengi huwa hawayasafishi.  Hawafikishi mswaki kwenye meno hayo.

Kinywa Kikavu

Kwa kawaida mate husaidia kusafisha kinywa na kuondoa mabaki ya chakula hivyo mtu mwenye kinywa kikavu huweza kuwa na harufu mbaya kutokana na upungufu huo.

Kwa kawaida kinywa kikavu hutokea usiku mtu anapolala na akiamka huwa na harufu ya asubuhi ambayo huongezeka iwapo mtu huyo alilala kinywa wazi.  Hali hii pia huweza kusababishwa na magonjwa ya tezi la mate matumizi ya baadhi ya dawa ambazo huathiri ufanyaji kazi wa tezi la mate.

Dawa

Baadhi ya dawa zinachangia harufu mbaya ya kinywa endapo zitasababisha ukavu wa kinywa.  Lakini kuna dawa nyingine zinapotumiwa kisha kumeng’enywa mwilini hutoa kemikali ambazo humfanya mtumiaji atoe harufu yake wakati wa kupumua.

Maambukizi Kinywa

Harufu mbaya inaweza kusababishwa na maambukizi hasa kwenye vidonda vilivyomo kinywani.  Vidonda hivi huweza kutokana na sababu mbalimbali, ikiwamo kung’oa jino kisha pengo likapata maambukizi.

Tumbaku

Uvutaji wa sigara au matumizi ya bidhaa zozote na tumbaku mfano ugoro au shisha huambatana na harufu ambayo mara nyingi huwa mbaya.  Wavutaji wa sigara wana uwezekano wa kupata ugonjwa wa fizi ambao ni chanzo kingine cha harufu mbaya.

Vyakula

Kuna baadhi ya vyakula huleta harufu isiyo nzuri kinywani.  Vyakula kama vile vitunguu maji, tangawizi na vinginevyo baada ya muda huleta harufu mbaya ya kinywa.

Magonjwa Mengine

Mara chache harufu mbaya ya kinywa huweza kusababishwa na maambukizi sugu ya tezi (chronictonsilitis) ambayo bakteria wanaosababisha pia huchangia harufu mbaya.  Halikadhalika maambukizi sugu kwenye pua na koo huweza kuchangia tatizo hili.

Saratani ya kinywa na koo na magonjwa yanayohusiana na mfumo wa chakula pia huweza kusababisha harufu mbaya ya kinywa.  Vilevile, kuna watu ambao hupata tatizo la tindikali ya tumboni kuja kwenye koo na kinywani (gastroesophageal reflux disease, GERD) nao wanaweza kupata tatizo hili.

Matibabu

Ili kuondokana na harufu mbaya ya kinywa, jikinge usipate matundu kwenye meno na jizuie na magonjwa ya fizi kwa kufanya vizuri usafi wa kinywa.

Kwa ujumla matibabu ya harufu mbaya ya kinywa hufanywa kwa kuishughulikia sababu hiyo endapo daktari atagundua kuchangiwa na ugonjwa fulani bado ataagiza utibiwe maradhi hayo kwanza.

Kuna mambo muhimu yanashauriwa ili kupunguza uwezekano wa kuwa na harufu hii.  Wataalamu wanaagiza kupiga mswaki meno ulimi walau mara mbili kila siku, asubuhi baada ya kula na usiku kabla ya kwenda kulala.  Mara baada ya kufanya hivyo, unapaswa kusukutua kwa dawa maalumu za kufanya hivyo (mouthwash).

Fanya flosi angalau mara moja kwa siku huku ukinywa maji mengi endapo una tatizo la kikavu kwani yanasaidia kupunguza tatizo hili.
Jitengenezee ratiba ya kumuona daktari wa kinywa na meno.  

Kumbuka kwa mtu wa kawaida inampasa kumuona daktari wa kinywa na meno mara moja kila baada ya miezi sita, yaani mara mbili kwa mwaka.  Lakini mwenye harufu mbaya unaweza kumuona mara nyingi zaidi na kufuata maelekezo yake.


This post first appeared on Afya Na Kiasi, please read the originial post: here

Share the post

HARUFU MBAYA YA KINYWA HAITIBIWI KWA DAWA ZA MENO

×

Subscribe to Afya Na Kiasi

Get updates delivered right to your inbox!

Thank you for your subscription

×