Get Even More Visitors To Your Blog, Upgrade To A Business Listing >>

Makala yangu ktk RAIA MWEMA la (leo) 06.01.16: Ubashiri wangu wa matukio yatakayojiri 2016

KWA miaka kadhaa, makala zangu za wiki ya mwanzo wa mwaka huzungumzia matukio mbalimbali yanayotarajiwa kutawala habari Katika mwaka husika. Makala hii ni mwendelezo wa utamaduni huo. Inajaribu kufanya ubashiri wa baadhi ya matukio yanayotarajiwa kujiri katika mwaka huu, ndani na nje ya nchi yetu.

Nianze na ubashiri wa matukio ya kimataifa. Mwaka huu ni wa Uchaguzi Mkuu nchini Marekani. Kwa kuzingatia mwelekeo wa kampeni zinazoendelea nchini humo, Ninabashiri Kuwa Hillary Clinton atafanikiwa kushinda kuwa mgombea urais kwa tiketi ya Chama cha Democrats, ilhali kuna uwezekano mkubwa wa Donald Trump kuibuka mgombea kwa tiketi ya Chama cha Republicans.

Hata hivyo, uwezekano huo unategemea mambo matatu muhimu. Kwanza, kwa wote wawili, nafasi zao kushinda au kushindwa zitategemea mwenendo wa uchumi wa taifa hilo kubwa duniani. Iwapo uchumi wa Marekani utaimarika zaidi, basi Hillary na chama chake watakuwa na fursa nzuri zaidi hasa kwa kutegemea uungwaji mkono wa Rais wa sasa wa nchi hiyo, Barack Obama, kujivunia rekodi ya uchumi chini ya chama chao. Uchumi ukiyumba, Trump, ambaye ni mfanyabiashara tajiri anaweza kuonekana kama chaguo sahihi kuwa rais ajaye wa nchi hiyo.

Jambo la pili, ambalo pia linawahusu wote wawili, ni hali ya usalama nchini humo. Iwapo hali itaendelea kuwa salama kama ilivyokuwa katika miaka minane ya Rais Obama, mgombea wa Democrats, ambaye ninabashiri atakuwa Hillary, atakuwa na nafasi nyingine nzuri ya kujivunia umahiri wa Rais kutoka Democrats kama Obama kulihakikishia usalama taifa hilo linalowindwa kwa udi na uvumba na vikundi mbalimbali vya ugaidi wa kimataifa. Iwapo kwa bahati mbaya kutatokea tukio lolote kubwa la ugaidi, basi hali hiyo yaweza kumnufaisha mgombea wa Republicans, ambaye ninabashiri atakuwa Trump, kwa kigezo chepesi tu kuwa Democrats wameshindwa kuiweka Marekani kuwa salama.

Jambo la tatu ni mwenendo binafsi wa wanasiasa hao wawili. Kwa upande wa Hillary, uwezekano wa yeye kuibuka mgombea wa Democrats utategemea uchunguzi unaoendelea kuhusu matumizi ya barua-pepe binafsi akiwa Waziri wa Mambo ya Nje. Japo Wamarekani wengi hawaonekani kuguswa na yaliyokwishafahamika kuwemo katika maelfu ya barua-pepe hizo, iwapo uchunguzi utabaini makosa makubwa zaidi, basi nafasi ya mwanamama huyo anayewania kuwa rais wa kwanza mwanamke wa taifa hilo itakuwa finyu, na huenda akalazimika kujiondoa katika kinyang’anyiro hicho.

Kikwazo kingine kwa Hillary ni tuhuma zilizoibuka hivi karibuni zinazoashiria uhusika wake katika tenda inayoihusisha Kampuni ya Symbion ambayo inahusu mradi wa uzalishaji umeme nchini Tanzania. Japo alichofanya mwanasiasa huyo sio kitu cha ajabu katika siasa za Marekani na hata katika nchi nyingine, ikigundulika kuwa taratibu zilikiukwa ili kupendelea marafiki zake, anaweza kuathirika vibaya na pengine kulazimika kujiondoa katika harakati zake za urais.

Wasiwasi mkubwa kuhusu Trump ni ile tabia yake ya kuwa kama bomu lililotegeshwa kwa muda (time bomb). Pamoja na kuendelea kung’ara katika kura za maoni miongoni mwa ‘wagombea’ wa Republicans, mwanasiasa huyo hana upungufu wa vioja, na fursa yake ya ushindi itategemea sana jinsi atakavyodhibiti mdomo wake kati ya sasa na wakati wa mchakato rasmi wa chama chake kuteua mgombea. Na hata akiruka kikwazo hicho, bado kuna wasiwasi iwapo Wamarekani watakuwa tayari kumchagua mwanasiasa asiyetabirika. Na endapo watamchagua, basi taifa hilo linaweza kutengwa na nchi nyingi duniani.

Iwapo Hillary hataibuka mshindi kwa tiketi ya Democrats, Ninabashiri Kuwa nafasi hiyo itakwenda kwa Bernie Sanders, ambaye hata hivyo ana nafasi finyu kumshinda mgombea yeyote atakayepitishwa na Republicans. Na iwapo Trump hatopitishwa, ninabashiri mbadala wake kuwa aidha Ted Cruz au Marco Rubio.

Katika anga hizo za kimataifa, ninabashiri kuwa hali nchini Burundi itakuwa mbaya zaidi ya ilivyokuwa mwaka jana. Kadhalika, ninabashiri hali ya usalama katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo kuzorota, hasa baada ya jitihada za Rais Joseph Kabila kutaka kuendelea kubaki madarakani.

Kadhalika, ninabashiri kuwa kundi la kigaidi la Boko Haram litaendelea kuisumbua Nigeria, huku kundi jingine la kigaidi la Al-Shabaab likiendelea kuzisumbua Somalia na Kenya. Pia kuna uwezekano wa kuwepo matatizo ya kisiasa huko Afrika Kusini na Zimbabwe yanayoweza kusababisha kung’oka madarakani kwa viongozi wa nchi hizo.

Habari za ugaidi wa kimataifa zinatarajiwa kuendelea kutawala anga za kimataifa huku makundi mawili hatari ya ISIS na Al-Qaeda yakiendelea kuwa tishio duniani, hususan nchi za Magharibi.

Kadhalika, ninabashiri kuwa eneo la Ghuba na Mashariki ya Kati kuingia katika mgogoro mkubwa utakaoligawa eneo hilo kati ya Waislam wa madhehebu ya Sunni wakiongozwa na Saudi Arabia, na wale wa Shia wakiongozwa na Iran.

Kwa huko nyumbani, ninabashiri kuwa Rais Dk John Magufuli ataendelea na utumbuaji majipu, japo habari ninayobaishiri kuwa itatawala zaidi ni kuibuka kwa skandali mbalimbali zilizojitokeza wakati wa utawala wa Rais Jakaya Kikwete na ambazo umma haukuwahi kuzifahamu. Kimsingi, harakati za Dk. Magufuli kutumbua majipu zina kila ishara ya kukutana na madudu yaliyosheheni wakati wa utawala wa mtangulizi wake.

Kadhalika, ninabashiri uwezekano wa baadhi ya mawaziri au manaibu wao kufukuzwa kwa kushindwa kuendana na falsafa ya Hapa Kazi Tu. Kwa vile si vema kumwombea mtu mabaya, ninahifadhi majina ya mawaziri ninaodhani wanaweza kuwa waathirika wa awali.

Vile vile, ninabashiri uwezekano wa kuwepo jitihada za chini chini ndani ya CCM kukwamisha dhamira ya Dk. Magufuli kukabiliana na ufisadi, rushwa, ujangili, biashara ya dawa za kulevya, na maovu mengine. Hata hivyo, jitihada hizo hazitafanikiwa.

Kwa upande mwingine, ninabashiri kuwa Dk. Magufuli ataendelea kunga’ra ndani na nje ya nchi, na dunia itaelekeza macho yake nchini Tanzania kutokana na mafanikio makubwa ya kiuongozi na jitihada za kufufua na kuboresha uchumi.

Kingine ninachoweza kubashiri ni ujio wa sura mpya nyingi katika uongozi ngazi za mikoa na wilaya, huku ikitarajiwa kuwa kama ilivyokuwa kwa Baraza la Mawaziri na Makatibu wakuu, wasomi mbalimbali wakiteuliwa kushika nyadhifa za u-RC na u-DC.

Kwa upande wa vyama vya upinzani, ninabashiri uwezekano wa jitihada za kumng’oa Mwenyekiti wa taifa wa Chadema, Freeman Mbowe, japo haitakuwa jambo la kushangaza iwapo atanusurika. Kwa kiasi kikubwa, uhai wa kisiasa wa Mbowe utategemea uhusiano wake na aliyekuwa mgombea urais kwa tiketi ya Ukawa, Edward Lowassa.

Eneo ambalo ninashindwa kubashiri kwa uhakika ni hali ya kisiasa huko Zanzibar. Hata hivyo, ninaweza kubashiri bila uhakika kuwa CCM itafanikiwa kulazimisha marudio ya uchaguzi, na kuna uwezekano CUF wakasusia. Uwezekano mwingine ni kurejewa kwa kilichofanyika baada ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010, yaani kuundwa kwa serikali ya umoja wa kitaifa. Ubashiri sio sayansi timilifu (exact science) kwa hiyo nitahadharishe kuwa baadhi ya niliyobashiri yanaweza kuwa kinyume.

Ubashiri huu umetokana na kufuatilia kwa karibu siasa za kimataifa na za huko nyumbani.


Nimalizie makala hii kwa kuwatakia tena heri na baraka za mwaka mpya 2016. Kwa huko nyumbani (Tanzania), kuna kila sababu ya mwaka huu kuwa mzuri kutokana na dalili za awali za utawala wa Dk. Magufuli kuiondoa Tanzania yetu katika lindi la ufisadi na rushwa, vitu vilivyochangia mno kudumisha umasikini wa nchi yetu. Lakini ili afanikiwe, ni wajibu wa kila Mtanzania kutimiza ‘Hapa ni Kazi Tu’ kwa vitendo.




This post first appeared on KULIKONI UGHAIBUNI, please read the originial post: here

Share the post

Makala yangu ktk RAIA MWEMA la (leo) 06.01.16: Ubashiri wangu wa matukio yatakayojiri 2016

×

Subscribe to Kulikoni Ughaibuni

Get updates delivered right to your inbox!

Thank you for your subscription

×