Get Even More Visitors To Your Blog, Upgrade To A Business Listing >>

Mfanyabiashara Kiluwa Yamkuta Maxito Ikulu Mbele ya Rais Magufuli

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi amesema Serikali ilifuta hati ya umiliki wa eneo la ekari 1,000 iliyokuwa ikidaiwa kununuliwa na Kiluwa Group kwa sababu iliuzwa kinyume cha sheria.

Mbali na kuuzwa kinyume cha sheria, pia imethibitishwa kuwapo kwa udanganyifu mwingi katika kampuni hiyo ikiwemo kutomiliki viwanda bali kufanya kazi kama Kituo cha uwekezaji (TIC) kwa kuchukua ardhi na kukodisha kwa wengine.

Ameyasema hayo jana  Ijumaa 7, 2019 wakati akijibu ombi la Mkurugenzi wa kampuni hiyo, Mohammed Kiluwa aliyeomba aruhusiwe kufanya uendelezaji wa kujenga viwanda katika eneo hilo lililopo Mkoa wa Pwani, huku akiahidi kama atashindwa yuko tayari kufukuzwa nchini.

“Siku unafungua kiwanda changu uliniambia kama eneo nililokuwa nimepata limejaa naweza kuomba eneo lingine kwa Mkuu wa Mkoa, eneo lako kwangu lilikuwa ni agizo nilifanya hivyo na kuomba eneo la ekari 1000.

 “Nilipeleka maombi ofisini kwake na akatoa utaratibu wa kwenda Halmashauri ambako walinijibu na baadaye waliniambia nilipie nikatoa Sh. bilioni moja na kodi ya Sh milioni 200 na baada ya kukamilisha taratibu zote za sheria ya nchi nilianza kufanya taratibu za ujenzi.

“Cha kushangaza nimeanza kujenga kiwanda cha Saruji kikubwa nikaletewa barua kuwa nisimamishe ujenzi huo na barua hiyo inaeleza kuwa eneo hilo liko chini ya daftari ya rais. Ninakuomba lile eneo uniruhusu niendelee na uwekezaji.

“Nina kampuni nyingi ambazo nimeongea nazo na kukubaliana nazo, leo ukiniruhusu mimi kesho naanza ujenzi pale na ndani ya miezi minne uje ufungue viwanda 10 pale au zaidi na nilijipanga baada ya kushika kauli yako ya Tanzania ya uchumi wa viwanda.”

 “Nitajenga viwanda pale, nitajaza viwanda pale, na nisipofanya niko tayari hata kufukuzwa nchini,”alisema Kiluwa

Akifafanua kuhusu suala la ardhi ya Kiluwa baadae, Lukuvi ambaye alipewa nafasi ya kuzungumza kuhusu malalamiko yaliyoelekezwa kwenye wizara yake alisema waliomba kumiliki ekari 1000 katika halmashauri ya Kibaha kinyume na utaratibu.

“Wakati wanazungumza na Halmashauri ya Kibaha waliambiwa market value ya ekari moja ni shilingi milioni 5.8, lakini kwenye kikao walitetewa sana na mkoa na wakaambiwa msipowauzia kwa milioni moja Rais anaweza kuwapa bure kama alivyowapa watu Bagamoyo kwa hiyo wakawauzia kinyume na matarajio.

“Sijui kwa huruma au namna gani, mwenyekiti wa halmashauri, mkurugenzi, sekretari  wa mkuu wa mkoa na mtu mwingine wa uwekezaji walipelekwa China kwanza, waliporudi mambo yakabadilika na mambo mengine walirudi nayo, lakini haya mambo mengine nadhani mtu wa Takukuru atajua baadae,” alisema

Lukuvi alisema lakini baadae walikuja kuuza ardhi kinyume na matarajio ya bei ya soko ya shilingi milioni moja kwa ekari  na bado wakalazimisha wapewe  shamba lile.

“Kwa utaratibu  mashamba yote ambayo umeyafuta wewe Rais huwa hayapangwi wala hayauzwi tena na wilaya, wizara ndio inayosimamia upangaji wa ardhi kwa maelekezo yako,”.

 “Hii kampuni ya Kiluwa Free Processing Zone kwa mujibu wa taarifa za Brela za leo (jana), kuna mtu anaitwa Kamaka, huyu ni mrusi  ameishi nchini kwa miaka 25 ana hisa 6,500, Mohamed Kalua aliyekuwa naongea hapa ana hisa 1500, katika hili eneo wanaotaka kulichukua, watatu anaitwa Kiluwa Steel Group wanahisa 2000.

“Lakini ukipekuwa chini hawa ni wageni kutoka China, hawa wanaojiita Kiluwa steel group kuna wachina hapa ndani, na Mohamed ana hisa zake hapa 1500” alisema na kuongeza;

“ Kamaka huyu alikuja kwangu, huyu Kamaka Godfadher wake nchini ni Subash Patel, lakini huyu ni mrusi anafanya kazi na wanafabiashara wengi”, alisema, Lukuvi.

Alikuja ofisini kwangu akiwa na mfanyabiashara wa SGS  yeye ndiye aliyempa bilioni 4 kwa ajili ya kununulia eneo hilo lakini yeye alililipia  bilioni moja.

 “Pamoja na udanganyifu mwingi ulionekana, hawa hawana viwanda, waliwapeleka hawa watu  China wakawaonyesha wanaowekeza viwanda, wenyewe wapo.

 “Kamishna wangu na watendaji wangu wana akili sana na kwa kuangalia huu utendaji usiokuwa na mizengwe mizengwe na kwa msimamo wako hati hizi zimefutwa kwa sababu upatikanaji wake haukuwa wa haki,  Nataka nimwambie Mohamed Kalua umeshaandikiwa barua, umemtumia mkuu wa mkoa nimejibu, umemtumia mkurugenzi wa TIC nitamjibu, nataka nikwambie hapa mbele ya wafanyabiashara wenzako ardhi hii uliyopewa ni kinyume cha utaratibu”  alisema Lukuvi.

Baada ya kusikiliza hoja za Lukuvi, Magufuli alisema;

“Unajua mimi nilimshangaa huyu Kalua nilikuwa simjui lakini alipoanza kungumzia hili nikaona huyu shetani amempandia wapi, sera ya ardhi kwa mujibu wa sheria za ardhi sera ya mwaka 1965 imefafanua wazi kwamba ardhi itapewa kwa raia wa Tanzania tu ambaye siyo raia atapewa kupitia TIC kwa ajili ya uwekezaji hiyo ndiyo sheria.

“Lakini pia ukiisoma sheria namba 4 ya mwaka 1995 na sheria ya vijiji namba 5 ya mwaka 1995 na sheria ya matumizi ya ardhi kitu kinajulikana kabisa haiwezekani ukaenda ukachuka sijui ndiyo umarumbanja unachuka ardhi at acheap ‘price’

“Halafu unaanza kuiuza nilikwenda kuweka jiwe la msingi kufungua kile kiwanda cha ndugu Kalua na nilipofika tu nilijua huyu ndugu Kalua siyo yeye peke yake ila walikuwa ni wachina kwa sababu waliokuwa wananitolea maelezo ni wachina lakini nikanyamaza kwamba mtu ameshakula percentage (asilimia) yake hapa acha afanye ‘business’ (biashara) yake.

“Nilikuwapo nikakifungua kwa sababu ninachotaka mimi ni employment (ajira) kwa watanzania wether you are black, blue or red  (haijarishi wewe ni mweusi, blue au mwekundu kwa sababu tuna-create employment, (tunatengeneza ajira) serikali ita-collect revenue (itakusanya kodi) na kadhalika.

Kutokana  na hilo Rais Magufuli alisema ardhi hiyo Kalua hawezi kuipata na wala asimlaumu Lukuvi kwani yeye ndiye aliyeagiza ifutwe.




This post first appeared on MASWAYETU, please read the originial post: here

Share the post

Mfanyabiashara Kiluwa Yamkuta Maxito Ikulu Mbele ya Rais Magufuli

×

Subscribe to Maswayetu

Get updates delivered right to your inbox!

Thank you for your subscription

×