Get Even More Visitors To Your Blog, Upgrade To A Business Listing >>

Hatimaye Jecha Afunguka Kuhusu Kufuta Uchaguzi Zanzibar...

Baada  ya kimya kirefu, hatimaye Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC), Jecha Salum Jecha amefunguka na kuelezea kuwa uamuzi aliouchukua wa kufuta uchaguzi wa Zanzibar wa mwaka 2015 baada ya kubainika kuwa na dosari, ulifanyika kwa kufuata taratibu, kanuni, Sheria na Katiba ya Zanzibar.

Jecha aliyasema hayo wakati akihojiwa na kipindi cha Funguka, kinachorushwa na Kituo cha Televisheni ya Azam na kusisitiza kuwa, hana wasiwasi wala hofu yoyote kwa hatua hiyo, aliyoichukua ya kufuta uchaguzi kwa kuwa ilifuata misingi yote ya Sheria na Katiba.

Pamoja na kwamba alikataa kujibu kwa undani kuhusu hatua yake hiyo na kusisitiza kuwa mengi atayabainisha kwenye taarifa ya tume, alisisitiza kuwa hakuwahi kutumika na chama chochote wala kuwasiliana na Rais Ali Mohammed Shein kama inavyodhaniwa na wengi.

“Haya yote yataonekana kwenye taarifa ya uchaguzi, siwezi kuongea hapa sasa ila kiukweli utaratibu ulifuatwa. Matokeo yalifutwa kutokana na dosari zilizojitokeza ikiwemo baadhi ya matokeo kujulikana kabla na kusababisha baadhi ya vyama kulalamika,” alisisitiza Jecha.

Alieleza kuwa matatizo na dosari za uchaguzi huo, yalianza kujitokea katika kipindi cha kupokea matokeo ambapo matokeo yalitoka katika maeneo ya Unguja, hayakubainika kuwa na matatizo, isipokuwa kwa matokeo yalitoka katika maeneo ya Pemba.

Alisema katika kura hizo za Pemba, ilibainika kuwa utaratibu wa kiufundi ulifanyika kuharibu matokeo ya hesabu za kura baada ya kufanyika urekebishaji wa kasoro wa mambo, ambayo hayakutakiwa yafanywe nje ya sheria za uchaguzi.

Alisema baada ya kutokea kwa dosari hizo, kwa upande wa tume kupitia yeye, iliamua kufuta uchaguzi mzima ili kuepusha vurugu na mgongano wa kisiasa huku Polisi ikifanya uchunguzi kuwabaini wahusika waliosababisha dosari hizo katika matokeo ya uchaguzi.

Kuhusu kushirikisha wajumbe wengine wa tume katika kufanya maamuzi ya kuufuta uchaguzi, Jecha alibainisha kuwa tume nzima ya ZEC ilihusika katika kufutwa kwa uchaguzi huo na ndio maana baada ya kufutwa taratibu za uchaguzi mwingine zilitekelezwa vyema na tume hiyo.

Hata hivyo, alibainisha kuwa katika kutangaza uamuzi wa kufuta uchaguzi huo, alilazimika kufanya hivyo binafsi baada ya kuona hali ya matokeo hayo inazidi kuwa mbaya na kwenda kinyume cha taratibu za uchaguzi.

Alibainisha kuwa baada ya kufuta uchaguzi huo, ili kuleta usawa kwa vyama vyote, tume hiyo ilisubiria vikao vya kutafuta mustakabali wa kisiasa visiwani humo vilivyokuwa vikifanyika baina ya viongozi wa kisiasa wa vyama vyote ndipo itangaze tarehe ya uchaguzi mpya.

“Tulikaa kimya kwa takribani mwezi mmoja tukisubiri hatua zichukuliwe na viongozi kupitia hivyo vikao vyao. Tulisubiri katika ule muda bila kuvunja sheria, na baada ya kuona hakuna hatua zinachokuliwa dhidi ya maamuzi yetu tulitangaza tarehe ya uchaguzi,” alieleza Jecha.

Mwenyekiti huyo alikanusha madai kuwa ametumika kufuta uchaguzi huo kwa maslahi ya CCM na Dk Shein. “Hapana, Sijawahi hata mara moja kuitwa au kutafutwa na kiongozi yeyote wa serikali, wala Rais sijawahi kuwasiliana na hata namba yake sina,” alifafanua.

Alisema ingawa hajawahi kukutana na mtu yeyote anayemlaumu kuhusu uamuzi wa tume hiyo wa kufuta uchaguzi, endapo kuna mtu bado ana malalamiko, anaruhusiwa kuiandikia ZEC malalamiko yake na si yeye binafsi, yatafanyiwa kazi.

Pamoja na hayo, mwenyekiti huyo alisisitiza kuwa hata baada ya kuufuta uchaguzi huo, kwa kuwa anaamini alifuata taratibu na sheria zote, hakujificha wala kuogopa kitu, kwani aliendelea na shughuli zake kama kawaida.

“Hadithi zilikuwa nyingi, kila mmoja alifikiri alivyotaka yeye, mie nilikuwepo Zanzibar natembea, lakini si kila mtu alikuwa ananiona. Redio za kijamii kila moja ilikuwa inazungumza vyake, mwenyekiti yuko hivi, mwenyekiti yuko wapi, mwenyekiti kesho ananyongwa mara nimepelekwa mahakama za kimataifa yote hayo yalizungumzwa lakini mie nipo,” alisema.


This post first appeared on MASWAYETU, please read the originial post: here

Share the post

Hatimaye Jecha Afunguka Kuhusu Kufuta Uchaguzi Zanzibar...

×

Subscribe to Maswayetu

Get updates delivered right to your inbox!

Thank you for your subscription

×